2013-08-09 14:41:18

Msamaha ni hatua muhimu katika mchakato wa upatanisho wa kweli!


Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, Ijumaa tarehe 9 Agosti 2013 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu, ikishirikiana na Baraza la Maaskofu Katoliki Japan, kama sehemu ya kumbu kumbu ya wahanga wa Vita kuu ya Pili ya Dunia.

Japan inakumbuka tarehe 9 Agosti 1945 mji wa Nagasaki ulipolipuliwa kwa bomu la atomic na hivyo kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Kardinali Turkson anasema kwamba, msamaha ni hatua muhimu sana katika mchakato wa kujipataanisha na hatimaye kudumisha amani ambayo kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomwajibisha mwanadamu.

Mwanadamu akishirikiana kwa ukamilifu na mpango wa Mungu, amani ya kudumu na endelevu inaweza kutawala katika mioyo ya watu. Kumbe, kuna haja kwa kila mtu kisimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki, amani na upendo, ili watu waonje pia huruma ya Mungu.

Kardinali Turkson anasema, kwa njia ya Yesu Kristo Mwenyezi Mungu ameweza kujipatanisha na wanadamu, mwaliko kwa waamini kutubu na kumwongokea Mungu, huku wakionesha moyo wa unyenyekevu na kwamba, Mwenyezi Mungu ndiye anayeweza kumkirimia mwanadamu furaha na amani ya ndani kama Kristo mwenyewe anavyofafanua katika Heri nane za Mlimani.

Utajiri na umaarufu wa mtu ni mambo ya mpito kamwe hayawezi kuzima kiu na njaa inayobubujika kutoka katika undani wa mtu. Yesu mwenyewe amewafundisha wafuasi wake kwa kusema kwamba, amani ya kweli ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Kila mwamini ajibidishe kutafuta amani kwa njia ya sala na ushuhuda wa maisha yake kama mfuasi amini wa Kristo.

Kwa Ibada ya Misa Takatifu na Baraza la Maaskofu Katoliki Japani, Kardinali Peter Turkson amehitimisha ziara yake ya kikazi nchini Japan kama sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 68 tangu Japan iliposhambuliwa kwa mabomu ya Atomic na kusababisha maafa makubwa katika miji ya Hiroshima na Nagasaki.







All the contents on this site are copyrighted ©.