2013-08-08 08:32:05

Vijana msijifanye kuwa "bize" kiasi hata cha kukosa muda wa majitoleo kwa wale wanaowazunguka! Noma hiyo!


Queen Said Mratibu wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio nchini Tanzania katika mahojiano na radio Vatican anasema kwamba, alipokuwa chuoni alijiunga na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio baada ya kuguswa na moyo wa huduma na majitoleo yaliyokuwa yanafanywa na wanachama hao. RealAudioMP3

Anasema, kwa njia ya Jumuiya, kijana anaweza kugundua shida na mahangaiko ya watu wanaomzunguka, akaguswa na kubadilishwa mintarafu mwanga wa Injili.

Anasema, falsafa inayoongoza maisha yake ni kujitosa kimasomaso kwa ajili ya wengine, hasa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii na kwa njia hii ameonja neema na baraka tele katika hija ya maisha yake ya ujana. Anasema, kuna faida kubwa kwa kijana anapojitoa kwa ajili ya kuwahudumia wengine na kwamba, muda ni zawadi ambayo kila kijana amebarikiwa kuwa nayo, jambo la msingi ni kuangalia jinsi ambavyo kijana anavyoutumia muda wake. Vijana wanadhani kwamba, wako "Bize" kiasi cha kukosa muda kwa ajili ya jirani zao, jambo hili si kweli!

Queen Said anasema kwamba, kundi la waamini walei na hasa vijana ni kubwa sana ndani ya Kanisa, ikilinganishwa na Makleri au watawa, kumbe waamini walei wanahamasishwa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa, kwa njia ya ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, ili kuyatakatifuza malimwengu. Kwa namna ya pekee kabisa, vijana waoneshe ile furaha ya kuwa ni mfuasi wa Kristo.

Vijana wajitahidi kufanya kazi halali na waendelee kufungua akili na miyo yao ili kuguswa na shida pamoja na mahangaiko ya watu wanaowazunguka kama anavyoendelea kukazia Baba Mtakatifu Francisko. Queen Said anasema, Baba Mtakatifu anawapenda na kuwathamini vijana, anawatuma kuwa ni mashahidi na wadau wa Uinjilishaji Mpya kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Ni changamoto kwa vijana kuachana na uvivu na tabia ya kupenda kubweteka!

Anatumia fursa hii pia kuwakaribisha vijana wanaojisikia kuguswa na shida pamoja na mahangaiko ya jirani zao, kujiunga na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio ambayo inatekeleza utume wake katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.







All the contents on this site are copyrighted ©.