Kheri na baraka katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Id El Fitri
Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa waamini wa dini ya Kiislam, kilikuwa ni kipindi cha
kufunga, kusali na kutoa sadaka. Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza amewaandikia
waamini wa dini ya Kiislam salam na matashi mema wanapoadhimisha Siku kuu ya Id El
Fitri. Kauli mbiu ya salam hizi ni kuhamasisha hali ya kuheshimiana kwa njia ya elimu.
Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini
anasema, ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa waamini wa dini ya Kiislam wakati
huu wanapoadhimisha Siku kuu ya Id El Fitri unaonesha jinsi ambavyo anaendelea kutoa
kipaumbele cha pekee katika kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini na waamini wa
dini ya Kiislam, kama alivyokuwa anafanya wakati wa maisha na utume wake nchini Argentina.
Anasema,
waamini wa dini hizi mbili wanapaswa kujenga na kuimarisha utamaduni wa kuheshimiana
na kuthaminiana katika masuala ya: Imani na Nyumba za Ibada, dhamana ambayo inapaswa
kutekelezwa zaidi na viongozi wa dini zote mbili kwa kutoa majiundo makini kuhusu
imani zao.
Kanisa Katoliki bado linaendeleza mchakato wa majadiliano ya kidini
bila ya kukata tamaa hata kama matokeo yake bado hayajaridhisha sana. Waamini wa dini
hizi mbili watambuane kwamba, wako katika hija ya kumtafuta Mwenyezi Mungu mintarafu
imani zao na wala kamwe si maadui wanaosigana mara kwa mara hata katika mambo ya kawaida.
Serikali
na wananchi wa Ulaya wanapaswa kujielimisha zaidi kuhusu Uislam na dini ya Kiislam;
kupambanua kwa kina na mapana tofauti kati ya imani na waamini wenye misimamo mikali
ya kiimani. Kila mtu anao uhuru wa kuabudu na kushuhudia imani yake, kwa kuheshimu
na kuthamini pia dini za wengine. Uelewa huu wa kina anasema Kardinali Tauran ni jitihada
ambazo zinapaswa kufanyika kuanzia katika familia, shule na kwenye taasisi za elimu
ya juu.
Waamini wa dini mbali mbali wajenge utamaduni wa kuheshimiana na kuthaminiana;
kupendana na kusaidiana daima wakikuza urafiki unaopania kuendeleza mchakato wa majadiliano
ya kidini, ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi. Bila urafiki wa
dhati, hakuna uwezekano wa kufanya majadiliano ya kweli!
Kardinali Tauran anasema,
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, amekuwa na mchango mkubwa katika
mchakato wa majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam katika utume wake.
Amebahatika kutembelea Misikiti mikubwa mitatu. Hii ndiyo njia na hamu ya Papa Francisko
anayotaka kuendeleza katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro,
ili waamini wa dini hizi mbili waweze kufahamiana, kuheshimiana na kupendana zaidi.
Baba
Mtakatifu tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, amebahatika kukutana na
viongozi mbali mbali wa dini ya Kiislam. Amewaonesha moyo wa upendo na ukarimu, anatambua
matatizo na changamoto zilizoko mbele yao, kwa pamoja wanaweza kushikamana na kusonga
mbele kwa imani na matumaini . Kuna baadhi ya nchi ambazo waamini wa dini ya Kiislam
wanabaguliwa kwa misingi ya imani, kama ilivyo pia hata kwa Wakristo katika baadhi
ya nchi.
Ili kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, urafiki na upendo
kati ya waamini wa dini ya Kiislam na Kikristo, kuna haja kwa vyombo vya habari kuwa
makini katika kuhabarisha, lakini kabla ya kuhabarisha, inawabidi wajifunze zaidi
ili kile watakachosema na kuandika, kiwe ni kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi.
Watu waondokane na ujinga wa kutofahamu mambo, hali ambayo wakati mwingine inasababisha
kinzani na migogoro ya kidini na kitamaduni.
Kardinali Jean Louis Tauran, Rais
wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini anahitimisha mahojiano na Radio Vatican
kwa kusema kwamba, kuna haja ya kutoa kipaumbele cha kwanza katika mambo mema na mazuri
yanayowaunganisha watu katika mshikamano wa upendo badala ya kuendelea kukazia mambo
ya misimamo mikali ya kidini, ingawa ni jambo ambalo ni la hatari katika maisha, ustawi
na maendeleo ya nchi yoyote ile.