Epukeni utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu; simameni kidete kujenga
amani ya kweli inayobubujika kutoka moyoni!
Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, Alhamisi tarehe
8 Agosti, 2013 ameshiriki katika Ibada ya Sala kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea
wahanga wa Vita kuu ya Pili ya Dunia, lakini kwa namna ya pekee, wale waliofariki
dunia hapo tarehe 9 Agosti 1945 kwa bomu la atomic lililorushwa mjini Nagasaki. Ibada
hii imefanyika kwenye Uwanja maarufu "Ground Zero Park".
Katika Ibada hii,
Kardinali Turkson amewakumbuka na kuwaombea binadamu wote wanaoendelea kuteseka katika
vita, njaa na magonjwa; amewakumbuka wahamiaji na wakimbizi; wahanga wa maafa na majanga
asilia pamoja na wale wote wanaonyanyasika na kudhulumiwa, katika ulimwengu wa utandawazi
usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya watu wengine. Hii ndiyo changamoto iliyotolewa
na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipotembelea Kisiwa cha Lampedusa.
Kardinali
Turkson ameendelea kusali pia kwa ajili ya wananchi wa Japan wanaoendelea kuathirika
kutokana na mionzi ya Nyuklia, mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kujenga utamaduni
wa haki na amani, ili Jamii ziondokane na wasi wasi wa mashambulizi ya silaha za kinyuklia.
Ni matumaini yake kwamba, waamini na watu wote wenye mapenzi mema, wataendelea kutembea
katika mwanga wa upendo wa Mungu, ili kuondokana na vitendo vya uvunjaji wa misingi
ya haki na amani na kamwe watu wasiendelee kuomboleza kutokana na vita.
Kardinali
Turkson anamwomba Bikira Maria Malkia wa Amani nchini Japan kuwasaidia waamini kutambua
kwamba, amani ya kwanza wanayopaswa kuitafuta ni kuondoa dhambi kutoka mioyoni mwao;
ili wakiwa safi na huku wamejipatanisha na Mungu pamoja na jirani waweze kuwa kweli
ni vyombo vya ujenzi wa amani, wakitoa fursa pia kwa Roho Mtakatifu kutekeleza kazi
yake kama sehemu ya mchakato wa mwendelezo wa kazi ya Ukombozi iliyoanzishwa na Yesu
Kristo mwenyewe, Bwana na Mfalme wa Amani.