Utamu wa imani shirikishi inayojionesha miongoni mwa vijana! Yaani, we...!
Kardinali Oscar Andrès Rodriguez Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Mashirika ya Misaada
ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis anasema, Maadhimisho ya Siku
za Vijana Duniani ni nyenzo kubwa katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa
mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.
Kwa mwaka
huu, vijana na watu wenye mapenzi mema, wameonja uzuri wa zawadi ya imani shirikishi,
vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, walipokusanyika mjini Rio de Janeiro, Brazil
kusherehekea zawadi ya imani na Baba Mtakatifu Francisko.
Brazil imeonesha
chemchemi ya matumaini mapya kutoka Amerika ya Kusini. Matukio ambayo yamewaacha vijana
wengi wakiwa wamepigwa na butwaa katika hija ya maisha yao ya imani ni katika Kesha
la kufunga Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.
Vijana
walijiandaa kikamilifu kwa tukio hili kwa kujitakatifuza katika Sakramenti ya Upatanisho,
wakamfuata Yesu kwa tafakari ya kina wakati wa Njia ya Msalaba iliyojaa utajiri mkubwa
wa changamoto zinazowakabili vijana katika maisha yao hapa duniani, mwishoni, vijana
wengi waliweza kushiriki Fumbo la Ekaristi Takatifu, chanzo na kilele cha maisha na
utume wa Kanisa. Licha ya umati mkubwa wa vijana kwenye Ufuko wa Copacabana, lakini
walionesha ibada na uchaji mkuu wakati wa kuabudu Sakramenti ya Ekaristi Takatifu.
Bado vijana wengi wanalikumbuka tukio kama hili wakati wa Maadhimisho ya Siku
ya 27 ya Vijana Duniani kwa mwaka 2011 iliyofanyika Jimbo kuu la Madrid, Hispania,
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita alipoamua kubaki na bahari ya vijana
iliyokuwa inanyeeshewa na mvua, kiasi kwamba, hata yale mahubiri yake yakalowa chapachapa
kwa matone ya mvua! Huu ni ushuhuda wa imani kwa Yesu wa Ekaristi Takatifu, mkate
wa uzima, ulioshuka kutoka mbinguni, chakula cha wasafiri.
Kardinali Maradiaga
anaendelea kusema kwamba, Makongamano ya Ekaristi Takatifu katika ngazi ya Parokia,
Kijimbo, Kitaifa au Kimataifa yamekuwa na mvuto mkubwa katika maisha ya waamini wengi.
Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu kwenye ufuko wa Copacabana, ilikuwa na mvuto wa
pekee, kutokana na uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko ambaye anaendelea kuwa ni kipenzi
cha wengi.
Maadhimisho ya Siku za Vijana ni nyenzo inayowasaidia vijana na
waamini kwa ujumla kugundua furaha ya imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Ni chemchemi
ya miito mbali mbali ndani ya Kanisa na mwaliko kwa vijana kujenga na kuimarisha umoja
na mshikamano miongoni mwao na Kanisa katika ujumla wake. Waamini walioshiriki kwa
namna moja au nyingine tangu kuanzishwa kwa Maadhimisho haya na Mwenyeheri Yohane
Paulo wa pili, wameendelea kuwa ni msaada mkubwa kwa maisha na utume wa Kanisa.
Kardinali
Maradiaga anasema, hata wale ambao imani yao ilikuwa inaanza kuota ukutu na ukakasi
wa maisha ya kiroho, wameweza kupata tena cheche za matumaini ya kuanza upya na hija
ya maisha yao ya kiroho! Huu ndio utamu wa imani shirikishi inayojionesha kwa namna
ya pekee miongoni mwa vijana.
Kila mahali ambapo Maadhimisho haya yamefanyika,
hapo waamini na watu wenye mapenzi mema wameshuhudia neema na baraka za Mungu kwa
ajili ya watu wake. Hizi ni nyakati zinazoleta ari na mwamko mpya katika imani, matumaini
na mapendo, fadhila za Kimungu. Waamini kwa namna ya ajabu wanapata mvuto na mguso
wa cheche za Injili wanapokutana na vijana wakitembea makundi kwa makundi katika miji
yao si haba.
Kardinali Oscar Maradiaga anasema, kwa mwaka huu, Rio wengi wanasema
imefunika! Hii inatokana na ukweli kwamba, Baba Mtakatifu Francisko alijimwaga miongoni
mwa wananchi wa Brazil bila ya hofu wala mashaka. Akawa tayari kuwanyooshea mikono
wote waliotaka kumsalimia! Hakuwa na wasi wasi wa kupokea na kunywa kile watu ambacho
walimpatia kwa moyo wa upendo na ukarimu! Haya ni matendo yanayobakiza chapa katika
maisha ya watu!
Ni maneno, matendo na ushuhuda unaowaachia watu wengi matumaini
mapya katika maisha yao. Kanisa linaendelea kumshukuru Mungu kwa uwepo wa Papa Francisko
ambaye anaendelea kulipyaisha Kanisa na kulifanya kuishi kipindi cha neema, mwaliko
kwa kila mwamini kutekeleza wajibu wa kumshuhudia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka
kutoka wafu kwa maneno na matendo adili!
Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.