Uhakika wa usalama wa chakula unapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza!
Jumuiya ya Kimataifa inapoendelea kukabiliana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa
pamoja na mabadiliko ya tabia nchi, kuna haja kwa wadau wa sekta ya kilimo kuhakikisha
kwamba, wanatoa kipaumbele cha kwanza katika uzalishaji wa chakula ili Jumuiya ya
Kimataifa iweze kuwa na uhakika wa usalama wa chakula.
Juhudi hizi
zinapaswa pia kuelekezwa katika mchakato wa upandaji na utunzaji wa misitu pamoja
na uvuvi bora, kwa lengo la kutaka kuwa na uhakika wa usalama wa chakula, jambo ambalo
ni nyeti kwa wakati huu kutokana na idadi idadi kubwa ya watu kuendelea kuteseka kutokana
na baa la njaa duniani.
Mikakati ya Shirika la Kilimo na Chakula la Umoja
wa Mataifa, FAO zinaonesha kwamba, nchi wanachama zimeendelea kutoa kipaumbele cha
kwanza katika sekta ya kilimo, kama njia ya kuchochea maendeleo ya mwanadamu sanjari
na kuongeza tija na uzalishaji katika sekta ya kilimo.
Ni mchango uliotolewa
hivi karibuni na Askofu mkuu Luigi Travaglino, Mwakilishi wa Vatican kwenye Mashirika
ya Chakula na Kilimo ya Umoja wa Mataifa mjini Roma. Ni matumaini ya Vatican kwamba,
katika kipindi kijacho, msukumo zaidi utaendelea kutolewa kwa wadau wa sekta ya kilimo
kuwekeza zaidi katika shughuli za uzalishaji zinazotekelezwa na wakulima wadogo wadogo,
kama njia ya kupambana na umaskini unaowakabili wananchi wengi wanaoishi vijijini,
ili kuweza kupatambana na hali yao ya maisha, ili iweze kuwa bora zaidi.
Askofu
mkuu Travaglino anasema kuwa Vatican inaunga mkono juhudi ambazo Jumuiya ya Kimataifa
inaendelea kuzifanya kwa kutoa kipaumbele kwa maboresho ya sekta ya kilimo vijijini,
kwa kuwezesha familia za wakulima ili kupambana na ukosefu wa chakula na umaskini
wa hali na kipato! Vatican inatambua familia kuwa ni mahali ambapo tunu msingi za
kiroho, kiutu na kimaadili zinaritishwa kutoka kizazi kimoja hadi kizazi kingine.
Familia ni mahali ambapo Mapokeo hai yanatunzwa na kwamba, umefika wakati
kwa wanawake ndani ya Jamii kuwezeshwa kikamilifu ili waweze kutekeleza wajibu wao
katika shughuli za kilimo. Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa limeutenga
Mwaka 2014 kuwa ni Mwaka wa Familia Kijijini. Kanisa Katoliki katika mikakati yake
ya kichungaji limeendelea kutoa kipaumbele cha pekee kwa watu wanaoishi vijijini pamoja
na kuonesha uwepo wake katika utekelezaji wa mikakati ya maendeleo vijijini.
Mwendelezo
wa mfumo wa chakula unaogusa kwa namna ya pekee masuala ya teknolojia, utunzaji wa
rasilimali na ubadilishanaji wa habari, hauna budi kuwashirikisha wakulima wadogo
wadogo vijijini, katika kupanga na kutekeleza mikakati ya shughuli za maendeleo ya
kilimo, ili kweli wakulima vijijini waweze kuchangia katika uzalishaji wa chakula
cha kutosha, kikolezo cha maboresho ya hali ya maisha na maendeleo ya wakulima vijijini
pamoja na kuendelea kutekeleza dhamana ya kuwa na uhakika wa chakula kwa kizazi kijacho.
Askofu mkuu Luigi Travaglino wakati akichangia kwenye mkutano wa 38 wa FAO
uliohitimishwa hivi karibuni mjini Roma, anaendelea kubainisha kwamba, miongozo maalum
itolewe kwa wahusika kutokana na ukosefu wa hali ya usalama wa chakula au pale ambapo
kuna idadi kubwa ya watu wanaoteseka kutokana na utapiamlo na lishe bora.
Athari
za myumbo wa uchumi kimataifa, zisiifanye Jumuiya ya Kimataifa kushindwa kuangalia
vipaumbele vingine katika kupanda na kuhifadhi misitu, uvuvi na biashara katika sekta
ya kilimo. Majadiliano ya wadau mbali mbali yajadili na kulenga mambo msingi yanayopania
kuwa na uhakika wa usalama wa chakula na wala si kwa ajili ya wajanja wachache kujipatia
utajiri na faida kubwa! Bei kubwa ya mazao ya chakula yana athari kubwa kwa wengi,
lakini kwa namna ya pekee kwa watu wanaoishi katika Nchi changa zaidi duniani.
Wakulima
katika nchi zinazoendelea wanapaswa kusaidiwa ili kuzalisha chakula cha kutosha na
ziada kuiuza kwenye soko la kimataifa. Yote haya anasema Askofu mkuu Luigi Tragavaglino,
Mwakilishi wa Vatican kwenye Mashirika ya Kilimo na Chakula yanapasa kuzingatia kanuni
maadili; mshikamano unaoongozwa na kanuni auni katika kupanga na kutekeleza mikakati
hii, ili Jumuiya ya Kimataifa iweze kufurahia amani na utulivu!