2013-08-07 10:00:08

Mkiandamana na Yesu pamoja na Mtakatifu Gaetano, nendeni mkawahudumie maskini!


Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe wa matashi mema kwa njia ya video kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema nchini Argentina katika kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Gaetano, msimamizi wa Argentina, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 7 Agosti. Maadhimisho ya Mwaka 2013 yanaongozwa na kauli mbiu "Yesu pamoja na Mtakatifu Gaetano twende kuwahudumia maskini".

Baba Mtakatifu anasema, licha ya umbali anapenda kutumia fursa hii kukutana nao, ili kwa pamoja waweze kukutana na Yesu pamoja Mtakatifu Gaetano ili kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Hawa ni watu wanaohitaji kushirikishwa na kuonjeshwa huruma na upendo katika shida na mahangaiko. Hapa kuna haja ya kukutana nao ana kwa ana, kama kielelezo makini cha maisha na mafundisho kutoka kwa Kristo, ambaye daima alijitosa kimasomaso kwa ajili ya maskini bila hata ya kujibakiza hata kidogo.

Hata katika kutoa sadaka kwa maskini, kuna haja ya kujenga utamaduni wa kuwaangalia, kuwajali na kuwathamini kama binadamu, changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuibua,kujenga na kukuza utamaduni wa kukutana na watu wanaowazunguka. Waamini wakumbuke kwamba, kuna watu wengine wanateseka pengine kuliko wao na kwamba, ni watu wanaohitaji kuonja huruma na upendo.

Baba Mtakatifu anawashukuru waamini na wananchi wa Argentina katika ujumla wao kwa kumsikiliza anapoendelea kuwahimiza kujenga dhana ya kukutana daima wakiwa wameandamana na Yesu pamoja na Mtakatifu Gaetano. Kwa njia ya ushuhuda huu wa maisha, wanaweza kuwa kweli ni kikolezo na mvuto wa toba na wongofu wa ndani. Mtu ambaye amekutana na kumkirimia mhitaji zaidi, moyo wake unakuwa na kupanuka kutokana na upendo.

Baba Mtakatifu anahitimisha ujumbe huu kwa njia ya video ambao umerushwa na vyombo mbali mbali vya habari nchini Argentina kwa kuwasihi ili waendelee kumwombea katika maisha na utume wake!







All the contents on this site are copyrighted ©.