2013-08-07 08:00:51

Benki ya Vatican katika utekelezaji wa mikakati yake kwa kuzingatia ukweli, uwazi, tija na ufanisi


Baba Mtakatifu Francisko akiziungumza na waandishi wa habari waliokuwa kwenye msafara wake amekazia umuhimu wa Benki ya Vatican kutekeleza dhamana na majukumu yake kwa kuzingatia: maadili, ukweli na uaminifu. Benki ya Vatican, IOR yaani “Istituto per le Opere di Religione” ilianzishwa tarehe 27 Juni 1942 na Waraka wa Kipapa, ikapewa jukumu la kuratibu masuala ya fedha kwa Vatican na wadau wake ndani ya Kanisa Katoliki sehemu mbali mbali za dunia. RealAudioMP3

Chimbuko la Benki hii ni wazo lililotolewa na Baba Mtakatifu Leo wa XIII kunako mwaka 1887, aliyeanzisha tume kwa ajili ya mafao ya Kanisa. Benki hii iliendelea kutekeleza majukumu yake, ikapambana na changamoto na kinzani mbali mbali.

Kunako Mwaka 1990 Mwenyeheri Yohane Paulo II akafanya marekebisho makubwa katika Katiba ya Benki ya Vatican, ili iweze kulinda na kuratibu mali na fedha ambazo zimekabidhiwa kwa Taasisi hii ya fedha kwa ajili ya shughuli za kidini na matendo ya huruma. Wafanyakazi na taasisi zinazotekeleza wajibu wake mjini Vatican zinaweza kuweka na kutunza fedha katika Benki hii. Ni Benki inayotekeleza wajibu wake kwa ajili ya Kanisa la Kiulimwengu kwa kulinda amana, rasilimali ya Kanisa pamoja na kutoa huduma za kibenki sehemu mbali mbali za dunia.

Ni Benki inayotoa huduma pia kwa: majimbo, Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, Taasisi za Kanisa Katoliki pamoja na wafanyakazi wa Vatican walioenea sehemu mbali mbali za dunia bila kuwasahau wanadiplomasia. Benki ya Vatican inatekeleza dhamana yake mjini Vatican peke yake.

Kutokana na takwimu zilizotolewa hadi kufikia mwishoni mwa Mwaka 2012, Benki ya Vatican ilikuwa inahudumia taasisi 5,200 za Kanisa Katoliki: yaani: Vatican na taasisi zake, Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume pamoja na Majimbo ambayo kwa pamoja yanaunda asilimia 85% ya akaunti zilizoko Benki ya Vatican, zenye thamani ya Euro Billioni 6.0 kati ya Euro Billioni 7.1 zinazohifadhiwa kwenye Benki ya Vatican.

Takwimu zinaonesha kwamba, kuna jumla ya wateja 13, 700: hawa ni Makleri, Watawa, Wafanyakazi pamoja na wafanyakazi wastaafu wa Vatican wanaopokea mishahara na pensheni zao za uzeeni pamoja na wanadiplomasia wanaowakilisha nchi na taasisi mbali mbali za kimataifa mjini Vatican. Kundi hili linaunda asilimia 15% ya akaunti za Benki ya Vatican zenye thamani ya Euro Billioni 1.1 kati ya Euro Billioni 7.1. Benki hii inaendelea kufuata: maadili, sheria na kanuni za Vatican na zile za Kimataifa kwa kuzingatia ukweli, uaminifu na uwazi.

Benki ya Vatican kwa sasa inaendelea kufanyiwa marekebisho makubwa kwa kusoma alama za nyakati pamoja na kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika masuala ya fedha, utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.








All the contents on this site are copyrighted ©.