2013-08-06 10:14:40

Kanisa linapaswa kutekeleza shughuli zake za kichungaji kitaaluma, kwa kuzingatia maadili, ukweli na uwazi!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari wakati akirejea kutoka Brazil kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 alikazia umuhimu wa taasisi za Kanisa kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia misingi ya maadili, ukweli, uwazi na uaminifu.

Hivi karibuni, Baraza la Maaskofu Katoliki Rwanda kwa kushirikiana na Shirika la Misaada la Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani, liliendesha semina maalum kwa ajili ya wafanyakazi wa Idara za Baraza la Maaskofu Katoliki Rwanda kuhusu matumizi sahihi na makini ya rasilimali ya Kanisa kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa Kanisa Katoliki nchini Rwanda.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Padre Cèlestin Hakizimana, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Rwanda alifafanua kuhusu utekelezaji wa mikakati ya shughuli za kichungaji za Baraza la Maaskofu Katoliki Rwanda kuanzia mwaka 2008 hadi mwaka 2017 zinazopania Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Kanisa Katoliki nchini Rwanda linataka kutekeleza shughuli zake za huduma kwa watu wa Mungu kitaalamu wala si kwa kubabaisha.

Padre Hakizimana amewakumbusha wanasemina kuhusu Mafundisho Jamii ya Kanisa na Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki juu ya matumizi sahihi ya rasilimali ya Kanisa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Watu wa Mungu. Wafanyakazi wa Kanisa wanapaswa kuzingatia kanuni, maadili, ukweli na uwazi katika matumizi ya rasilimali ya Kanisa, vinginevyo hata wao wanaweza kujikuta wakitumbukia katika kashfa ya ufisadi na ubadhilifu wa mali ya Kanisa kama inavyojitokeza katika Jamii nyingi kwa sasa.








All the contents on this site are copyrighted ©.