Mikakati ya shughuli za kichungaji Amerika ya Kusini, ili kukabiliana na changamoto
zilizopo!
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Brazil, tarehe 28
Julai 2013, alipata pia fursa ya kukutana na kuzungumza na Maaskofu 45 wanaounda Sekretarieti
ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu katoliki Amerika ya Kusini na Caribbeni, CELAM.
Baba Mtakatifu katika mazungumzo yake, alijikita zaidi katika Maadhimisho
ya Mkutano wa Tano wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini
uliofanyika mjini Aparecida. Kwa mara ya kwanza, mkutano huo uliadhimishwa kwenye
Madhabahu ya Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya asili wa Aparecida nchini Brazil., hapo
Mwezi Mei, 2007.
Baba Mtakatifu alianza hotuba yake iliyosheheni changamoto
kwa Shirikisho la Baraza la Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini, kwa kuzungumzia kwanza
kabisa mihimili iliyobainishwa na Mababa wa Aparecida wakati wa mkutano wao. Kwanza,
ulikuwa ni ushiriki wa Makanisa mahalia kwa njia ya: Sala, Tafakari, Ibada na Maadhimisho
mbali mbali yaliyowasindikiza Maaskofu wakati wa mkutano wao huko Aparecida.
Mkutano
huu ulianzisha mchakato endelevu uliokuwa unapania kuhakikisha kwamba, Kanisa linaendeleza
dhamana na utume wake wa kutangaza Injili ya Kristo huko Amerika ya Kusini. Baba Mtakatifu
amewakumbusha Maaskofu hao kwamba, huu ulikuwa ni mkutano wao wa kwanza kufanyika
chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Aparecida.
Baba Mtakatifu Francisko
anasema, utume na dhamana ya Kanisa Amerika ya Kusini una mielekeo mikuu miwili; kwanza
kabisa ni mbinu mkakati wa shughuli mbali mbali za kimissionari zinazotekelezwa na
Mama Kanisa Amerika ya Kusini. Pili ni mwelekeo wa utekelezaji wa utume huu katika
uhalisia wa maisha ya Makanisa mahalia.
Utekelezaji wa majukumu haya unahitaji
mabadiliko ya miundo mbinu ya Kikanisa kutoka katika mfumo wa sasa na kuanzisha mifumo
mipya kabisa, ili kuliwezesha Kanisa kusonga mbele kwa imani na matumaini zaidi. Huu
ni mchakato unaojikita katika undani wa maisha ya waamini, unaowaalika waamini kutubu
na kumwongokea Mwenyezi Mungu, kwa kujenga na kuimarisha ndani mwao ari na moyo wa
kimissionari.
Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake kwa Maaskofu wa Sekretarieti
ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini, amebainisha changamoto
kuu mbili zinazolikabili Kanisa katika mazingira ya Amerika ya Kusini; mosi ni Utume
wa Kimissionari unaolichangamotisha Kanisa kufanya mabadiliko ya ndani katika maisha
na utume wake, tayari kutoka kifua mbele ili kujadiliana na ulimwengu unaolizunguka.
Katika dhamana hii, kuna vishawishi vinavyoweza kujitokeza kwa kuugeuza Ujembwa
Injili kuwa na mwelekeo na sera za kisiasa; kishawishi cha kutaka kuifasiri Injili
nje ya Injili na uhalisia wa maisha na utume wa Kanisa. Kishawishi kingine ni kulifanya
Kanisa kuwa kama mashine ya kutekeleza miradi ya maendeleo kiasi cha kuligeuza Kanisa
kuwa kama NGO fulani hivi.
Katika mwelekeo huu, taalimungu inayoibuliwa ni
ile ya utajiri na ufanisi ambayo hatima yake inajikita katika mikakati ya shughuli
za kichungaji zinazofanywa na Mama Kanisa. Baba Mtakatifu anasema, kishawishi kingine
kikubwa kinachoendelea kujionesha Amerika ya Kusini ni hali ya Makleri kuona kwamba,
maisha na utume wao ni kama ajira, hali inayoonesha kwa namna ya pekee ukosefu wa
ukomavu na uhuru wa Kikristo hata miongoni mwa waamini wengi Amerika ya Kusini.
Baba
Mtakatifu akizungumza na Maaskofu wa CELAM, ameonesha dira na mwongozo unaopaswa kutekelezwa
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Amerika ya Kusini. Jambo la kwanza ni
kujenga na kuimarisha Utume wa Kimissionari, changamoto iliyotolewa na Mababa wa Aparecida.
Huu ndio utashi wa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Kanisa la Amerika ya Kusini kwa nyakati
hizi, licha ya kinzani na changamoto mbali mbali zinazoendelea kujitokeza. Utume wa
Kimissionari ni ari na mwelekeo endelevu, daima unaojitahidi kusoma alama za nyakati.
Jambo la pili anasema Baba Mtakatifu ni kutambua kwamba, Kanisa ni Taasisi
iliyoanzishwa na Kristo, ambayo inahamasishwa kutoka kwenda kutangaza Injili ya Kristo
hadi miisho ya dunia na wala isijitafute yenyewe, vinginevyo, taasisi hii itakuwa
ni kama mradi au NGO. Kwa mwelekeo huu, Kanisa linakuwa si tena mchumba mwaminifu
wa Kristo; Mhudumu wa Neno la Mungu na Mafumbo Matakatifu, linajikuta likiwa ”Askari
na Msimamizi”.
Baba Mtakatifu Francisko anakumbushia kwamba, Mkutano wa Aparecida,
ulilichangamotisha Kanisa Amerika ya Kusini kuwa ni: Mchumba mwaminifu wa Kristo,
Mama na Mtumishi mwaminifu; Mkolezaji wa imani na wala si mdhibiti wa imani miongoni
mwa waamini.
Jambo la tatu anaendelea kubainisha Baba Mtakatifu Francisko
ni mikakati miwili ya shughuli za kichungaji iliyoibuliwa na Mababa wa Aparecida.
Mikakati hii inatambua upekee wa Injili inayoweza kulisaidia Kanisa kujipima ikiwa
kama linaishi ile dhamana ya Umissionari, kwa kuwa karibu na kukutana na waamini katika
hija ya maisha yao ya kiroho na kiutu. Hizi ni njia ambazo Mwenyezi Mungu amezionesha
katika historia ya ukombozi, ili kuwachangamotisha waamini kujisikia kuwa ni sehemu
ya maisha na utume wa Kanisa. Baba Mtakatifu anasema, kipimo madhubuti ikiwa kama
Kanisa liko na linakutana na Waamini wake ni Mahubiri.
Jambo la tano, anasema
Baba Mtakatifu ni Maaskofu kutekeleza wajibu na dhamana yao ya kuongoza Familia ya
Mungu, ili kuonesha dira na njia makini ya kufuata na wala si kutawala. Maaskofu wanapaswa
kuwa ni wachungaji wema na waaminifu, watu ambao wanatambua shida na mahangaiko ya
watu wao. Askofu ni kiongozi ambaye hana budi kuwa kweli na fadhila ya: uvumilivu,
huruma, upole na unyenyekevu.
Watu ambao wanapenda kukumbatia ufukara na maisha
ya kiasi, wakiwa huru katika kutumia mali na rasilimali ambayo imewekwa mbele yao
na Mama Kanisa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Familia ya Mungu. Maaskofu waoneshe
unyofu wa ndani na wala kamwe wasijisikie kuwa ni ”Wafalme na miungu wadogo wanaoabudiwa”.
Ni watu ambao wanajitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa
bila ya kumezwa na malimwengu.
Askofu awe ni kiongozi anayejitaabisha kujenga
na kuimarisha umoja, upendo na mshikamano miongoni mwa Familia ya Mungu. Asimame kidete
kuwalinda waamini wake dhidi ya hatari zinazoweza kujitokeza katika safari ya maisha
yao ya kiroho na kiutu, lakini zaidi, kwa wale wanaotaka kuwapora matumaini kutoka
katika undani wa maisha yao. Askofu awe daima ni kiongozi anayewasha moto na mwanga
wa matumaini kwa waamini wake, akiongozwa na uvumilivu wa Mungu katika kuwaongoza
watu wake.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, Askofu anapaswa kuwa kati ya watu
wake katika mambo makuu matatu: daima awe mstari wa mbele, ili kuwaonesha dira na
njia ya kufuata ili wasitangetange na kuyumbishwa kiasi hata cha kutokomea porini.
Askofu awe nyuma ya waamini wake, ili kuhakikisha kwamba, hakuna aliyeachwa wala kusahaulika,
lakini zaidi, waamini wenyewe kama sehemu ya mchakato wa ukomavu wanaweza kujiongoza
wenyewe bila ya kuwa na lazima ya kufuatwa fuatwa hata kwa mambo ya kawaida.
Baba
Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa Sekretarieti ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu
Katoliki Amerika ya Kusini na Caribbean kwa kuwaambia kwamba, kwa sasa shughuli za
kichungaji zinatindikiwa na wongofu wa ndani, changamoto kwa viongozi wa Kanisa na
waamini katika ujumla wao, kusaidiana kuanza tena kwa moyo mkuu, kwa ajili ya ustawi
na maendeleo ya Kanisa Amerika ya Kusini.
Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa,
C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.