2013-08-02 11:13:28

Waandishi wa habari Wakatoliki wanachangamotishwa kuwa ni mashahidi wa Kristo Mfufuka!


Njia za mawasiliano ya jamii ni nyanja inayokabiliana na mabadiliko makubwa katika ulimwengu wa sayansi, teknolojia na kitamaduni hata katika maisha, utume na historia ya Kanisa.

Ni mchango wa Askofu mkuu Claudio Maria Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii katika hotuba yake ya ufunguzi wa Mkutano mkuu wa Waandishi wa habari Wakatoliki kutoka Amerika ya Kusini,(OCCLAC) uliofunguliwa hapo tarehe Mosi, Agosti na unafungwa, Jumamosi, tarehe 3 Agosti 2013.

Akizungumzia mikakati ya mawasiliano kwa mwaka 2013 hadi mwaka 2017, alisema kwamba, waandishi wa habari wanapaswa kuwa ni vyombo vya ujenzi wa utamaduni wa kukutana na watu, ili kubomoa vikwazo na vizingiti vinavyojitokeza katika ulimwengu wa mawasiliano ya jamii, kiasi kwamba, watu wanashindwa kuwasiliana barabara hata kama wako kwenye mitandao ya kijamii.

Watu washirikiane kwa dhati ili kutokomeza upweke hasi unaoendelea kusababisha madhara makubwa katika maisha, ustawi na maendeleo ya watu. Ikumbukwe kwamba, mwanadamu ndiye anayepaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika mawasiliano na wala si vyombo vya mawasiliano. Watu wajifunze kukutana na kuwasiliana ili wajenge umoja na mshikamano.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwachangamotisha waandishi wa habari kushirikisha utajiri wa imani yao kutoka kwa Kristo na Kanisa lake, lakini baada ya kukutana na Yesu katika: Maandiko Matakatifu, Sakramenti za Kanisa na kwa watu wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Bado kuna vikwazo vinavyoikabili sekta ya mawasiliano ya kijamii sehemu mbali mbali za dunia kwani kuna watu wanaendelea kupigania uhuru wa kujieleza na uhuru wa vyombo vya habari.

Vyombo vya habari vinavyomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa vinapaswa kuwa mstari wa mbele kusimama kidete kulinda na kutetea ukweli, utu na heshima ya binadamu; haki msingi za binadamu mintarafu kweli za Kiinjili, maadili na utu wema. Vyombo hivi anasema, Askofu mkuu Claudio Maria Celli, vinapaswa kuwatangazia watu wanaoishi pembezoni mwa jamii, Habari Njema ya Wokovu, kwa kutambua kwamba, Uinjilishaji unamgusa mtu mzima: kiroho na kimwili, ili kuiona na kuitambua ile sura na mfano wa Mungu katika maisha ya kila mwanadamu.

Waandishi wa habari Wakristo wasukumwe kutangaza tunu msingi za maisha ya kiutu, kimaadili mintarafu Mafundisho na Kweli za Kiinjili, daima wakiongozwa na dhamiri nyofu. Wawe ni watu wanaofanya tafakari ya kina, ili kuendelea kutafuta utekelezaji wa mapenzi ya Mungu katika maisha na taaluma yao kama waandishi habari Wakatoliki.

Ni matumaini ya Askofu mkuu Claudio Maria Celli kwamba, waandishi habari Wakatoliki kutoka Amerika ya Kusini, watakuwa ni mashahidi bora wa Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu!







All the contents on this site are copyrighted ©.