2013-08-02 11:48:37

Mradi wa kuwawezesha wasichana wasanii, Kenya waanza kutimua vumbi!


Mshiriki mmoja mashuhuri wa mashindano ya “Tusker Project Fame” yenye kuwahusisha wasanii chipukizi, Bi. Amileena Mwenesi sasa ameanzisha mradi wa kuwasaidia wanamuziki chipukizi wa kike nchini Kenya kutambua na kukuza vipaji vyao.

Mradi huo unaojulikana kama “Mafao ya Msichana” umewapatia nafasi wasichana sita kujiunga na mafunzo ya dhati ya majuma sita ambapo wanasaidiwa kunoa vipaji vyao vya uimbaji kama matayarisho kwa ajili ya kushiriki kwenye hafla ya wasanii itakayofanyika mnamo Agosti 17, 2013.

Lengo la mradi wa Mafaa ya Msichana ni kusaidia kunoa na kukuza vipaji vya wasanii wa kike walio na msimamo wa maadili. Wasichana sita ambao wamebahatika kuwa wa kwanza kufaidi mafunzo yaliyoandaliwa na mradi wa Mafao ya Msichana ni miongoni mwa wasichana walioweza kufikia fainali katika mchuano wa majaribio ya sauti yaliyoandaliwa na kampuni ya Liberate Agency, ambayo pia huwaunda wasichana wasanii ili waweze kufaulu kwenye malengo yao maishani, na hushirikiana na jitihada kama zile za Mafao ya Msichana ili kuwajengea vipaji wasanii chipukizi.

Mwanzilishi wa Mafao ya Msichana, Amileena Mwenesi anasema kwamba, Liberate Agency ni kampuni ya Sanaa inayowapa fursa wasanii chipukizi kuboresha picha na sauti zao katika harakati za kujijenga kisanii. Mradi huu umeteuliwa na kampuni ya Liberate Agency kwa mwaka 2013 katika juhudi za huduma kwa jamii inaonyesha jitihada za kampuni hiyo katika kuwaunda wasichana ili waweze Kujifunza, kufikiri, kujieleza, kuhusiana na wengine, na kujiheshimu vilivyo katika mambo yanayohusu taaluma, na hivyo kuyamudu maisha yao vyema.








All the contents on this site are copyrighted ©.