2013-07-31 09:20:44

Utunzaji bora wa mazingira na maendeleo endelevu ni kati ya mambo yanayopewa kipaumbele na Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani


Uhusiano kati ya mazingira na maendeleo endelevu kati ya binadamu wote umepewa kipaumbele cha pekee kwenye barua ya hivi karibuni iliyoandikwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani.
Barua hiyo, iliyowekwa sahihi na maaskofu Stephen Edward Blare, Rais wa Tume ya Kitaifa ya Haki na Maendeleo ya Watu na Richard Edmund Pates wa Tume ya Haki na Amani Kimataifa, imetumwa kwa mjumbe wa Uchumi wa Serikali ya Marekani, Balozi Michael Froman na inaashiria kwamba, katika nyanja za biashara, kuna uhitaji wa maadili yanayotokana na kuheshimu utu na hadhi ya binadamu.
Barua hiyo pia inasema kwamba, faida na lengo la ushirikiano wa kiuchumi vinapaswa kuwa ni uboreshaji wa maisha hasa ya wafanyakazi maskini, wanyonge pamoja na familia zao.
Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani pia linasema kwamba, kuna uhitaji wa kulinda na kudumisha hadhi na heshima ya binadamu kwa kuzingatia sio tu haki za kikazi, bali pia haki za watu mahalia, kushughulikia vyanzo vya tatizo la uhamiaji, kuendeleza watu wanaoishi vijijini pamoja na kutunza mazingira, kazi ya uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemkabidhi mwanadamu.
Pia makubaliano yoyote ya kiuchumi na kibiashara ni lazima yasaidie kupunguza deni la nje linalozikabili nchi maskini duniani, pamoja na kuzisaidia nchi hizo kukua na kushiriki kikamilifu kwenye maamuzi ya kiuchumi na kibiashara katika medani za kimataifa.








All the contents on this site are copyrighted ©.