Viongozi wa Makanisa nchini Zimbabwe wanawataka wananchi wa Zimbabwe kuhakikisha kwamba,
wanaombea amani na utulivu wakati wa mchakato mzima wa uchaguzi mkuu nchini humo unaofanyika
tarehe 31 Julai 2013, ili uweze kuwa huru na wa haki; huku amani na utulivu vikitawala.
Viongozi wa Makanisa wanawataka wananchi wa Zimbabwe kuonesha ukomavu wa kisiasa
na kidemokrasia kwa kuachana na vurugu pamoja na ghasia kama zile zilizojitokeza wakati
wa uchaguzi mkuu kunako mwaka 2008 na hivyo kuipelekea Zimbabwe kujikuta inaogelea
katika kinzani na migogoro ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.