2013-07-31 08:07:40

Miamba wawili wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican kutangazwa watakatifu!


Baba Mtakatifu Francisko baada ya kusikiliza na maoni ya Makardinali na Maaskofu wakuu ameamua kuitisha mkutano wa Makardinali utakaoridhia Kanisa kuwatangaza Papa Yohane wa Ishirini na tatu na Yohane Paulo wa Pili kuwa Watakatifu. RealAudioMP3

Hayo yamesemwa na Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu, mara baada ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni.

Baba Mtakatifu ameridhia kuchapishwa kwa hati zinazotambua miujiza iliyotendwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, miaka michache tu, tangu alipotangazwa kuwa ni Mwenyeheri. Mama Kanisa anapoadhimisha Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican sanjari na Mwaka wa Imani, anapenda kuwaweka Papa Yohane wa XXIII pamoja na Mwenyeheri Yohane Paulo II kuwa ni mifano hai ya kuigwa katika maisha na utume wa Kanisa.

Haya ni matunda ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, tukio la: Kiekuemene; Upendo na Amani ya Kiinjili; kielelezo makini cha Mama Kanisa anayemjali mwanadamu katika maisha yake yote; wakati wa raha na machungu, daima anapania kumkirimia imani, matumaini na mapendo. Mwenyeheri Yohane wa XXII alitambulikana kuwa ni Papa mwema, Baba wa Wakatoliki na wasioamini, aliwakumbatia wote na kuwabariki.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, katika hija zake za kichungaji sehemu mbali mbali za dunia, ametangaza kwa maisha na maneno yake Injili ya Upendo, Haki na Amani; amekuwa ni kielelezo cha udugu, umoja na mshikamano kati ya watu wa mataifa; kwa kuonesha ukarimu kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Kardinali Angelo Amato anasema, viongozi hawa wawili ni wadau wakuu wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, kwa pamoja wameonesha fadhila ya utakatifu wa maisha ya Kikristo mintarafu utume na mazingira waliyokutana nayo katika nyakati zao. Yohane XXIII alionesha ujasiri mkubwa kwa kuitisha Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na matunda ya Mtaguso huu yanaendelea kujionesha katika maisha na utume wa Kanisa.

Mwenyeheri Yohane Paulo wa II akamwilisha Mafundisho ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kwa kushirikisha karama na fadhila ambazo alikuwa amekirimiwa na Mwenyezi Mungu katika maisha yake: akakazia taalimungu, sheria za Kanisa na Katekesi. Yohane wa XXIII alianzisha mchakato wa mabadiliko ndani ya Kanisa, akayaita “Aggiornamento”, Yohane Paulo II akatekeleza kwa uaminifu mkubwa mawazo ya Mababa wa Mtagauso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Viongozi hawa wawili wametekeleza dhamana yao kama Makhalifa wa Mtakatifu Petro kwa umakini mkubwa, wote wakiwa na Ibada ya pekee kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa. Bikira Maria akawa ni kielelezo cha imani na ufuasi wa Kristo.

Kardinali Angelo Amato anasema, bila shaka wengi wanakumbuka lile tukio la ajabu lililotokea tarehe 13 Mei 1981, alipopigwa risasi kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, lakini akasalimika baada ya mateso na mahangaiko makubwa; tangu wakati huo, akatambua na kuuona ulinzi wa Bikira Maria katika maisha na utume wake!

Vijana waliokuwa wamekusanyika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, wakati walipokuwa wanamsindikiza Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili katika dakika zake za mwisho mwisho kabla ya kuitupa mkono dunia, waliposikia kwamba, amefariki, wakapiga kelele na kuandika, “Santo Subito”, atangazwe mara moja kuwa mtakatifu! Ni ushuhuda uliotolewa na watu hata kabla ya kuanza mchakato wa kumtangaza kuwa ni Mwenyeheri.

Kardinali Angelo Amato anasema kwamba, Kanisa limefuata hatua kwa hatua mchakato mzima wa kumtangaza Yohane Paulo wa pili kuwa Mwenyeheri, bila kuwa na haraka wala shikinikizo lolote! Kanisa linapenda kufanya mambo yake kwa busara na hekima!

Mama Kanisa katika kipindi cha Miaka ya hivi karibuni amebahatika kuwa na Kundi kubwa na Watakatifu, ambao wamekuwa ni viongozi wakuu wa Kanisa. Ni Mapapa walionesha hekina na utakatifu wa maisha. Hawa ni Pio XII; Yohane XXIII; Yohane I; Yohane Paulo II. Ni viongozi walionesha utakatifu wa maisha katika utume wao kama Makhalifa wa Mtakatifu Petro.

Kutokana na maisha yao ya utakatifu, bado wanakumbukwa, wanapendwa na kuthaminiwa na wengi. Kanisa bado linaendelea kuiangazia dunia kwa mwanga wa utakatifu wa wachungaji wake wakuu!

Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.