2013-07-31 15:26:37

Dodoma washerehekea miaka 10 ya Shule ya Awali ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola


Shule ya Msingi ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola, iliyoko Jimbo Katoliki la Dodoma inayoendeshwa na Wayesuit, inasherehekea miaka kumi tangu ilipoanzishwa ili kutoa nafasi hata kwa watoto wa wakulima Jimboni Dodoma kupata elimu bora itakayowasaidia kupambana na mazingira yao kwa sasa na kwa siku za usoni.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika Waraka wake wa kichungaji, Dhamana ya Afrika anabainisha kwamba, shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki Barani Afrika ni rasilimali ya thamani kwa majiundo ya watu tangu wakiwa watoto, ili kujenga na kudumisha mshikamano wa umoja, haki na amani. Ni mahali ambapo watoto wanafundishwa tunu msingi za kiutu na maisha ya Kiinjili, changamoto kwa Kanisa Barani Afrika kuwekeza zaidi katika sekta ya elimu kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Bara la Afrika.

Elimu ijikite katika ukweli wa maisha unaopania kujenga misingi ya haki, amani na upatanisho wa kweli pamoja na kuwasaidia watoto na vijana wa Bara la Afrika kutambua fursa na changamoto zilizoko mbele yao katika ujenzi wa nchi na Bara la Afrika kwa ujumla.

Katika mahubiri ya Misa ya shukrani kwa ajili ya Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 10 tangu Shule ya Msingi ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola, Jimbo Katoliki la Dodoma ilipofunguliwa rasmi na Askofu mstaafu Mathias Isuja Josefu, Padre Chesco Peter Msaga, Makamu Askofu Jimbo Katoliki Dodoma, amewataka waamini kujenga moyo na utamaduni wa shukrani kwa Mwenyezi Mungu kutokana na mapaji na zawadi mbali mbali anazowakirimia katika maisha.

Waamini watambue kwamba, mafanikio, mali, fedha na yote waliyo nayo wamejaliwa na Mwenyezi Mungu na wala si kwa bahati nasibu au kutokana na ujanja wao. Hivyo wanapaswa kujifunza kuwashirikisha na kuwamegea wengine utajiri kwa njia ya mshikamano katika matendo ya huruma na mafao ya wengi. Kwa njia hii wanaweza kuonesha moyo wa shukrani unaojikita katika mshikamano wa upendo.

Katika sherehe hizi, Dr. Rehema Nchimbi, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, alitumia fursa hii kuwaalika wadau mbali mbali wanaotaka kuwekeza katika sekta ya elimu mkoani Dodoma kujitokeza kwani kwa sasa Dodoma ina mvuto mkubwa na inaendelea kujitanua katika medani mbali mbali za maisha. Lengo la Tanzania ni kuhakikisha kwamba, watanzania wanapata msingi wa elimu bora itakayowasaidia kupambana na mazingira yao kikamilifu.

Dr. Rehema amewataka wazazi kuhakikisha kwamba, wanachangia kikamilifu katika huduma za elimu kwa watoto wao, kwani huu ndio urithi bora zaidi, sanjari na kuhakikisha kwamba, wanafuatilia ufanisi wa majiundo ya watoto wao: kitaaluma, kitu na kiroho. Wazazi wamehimizwa kushirikiana na walezi pamoja na walimu kwa ajili ya malezi ya watoto wao katika sekta mbali mbali za maisha.

Naye Sr. Euphrasia Mwingira, Mkuu wa Shule ya Awali ya Mtakatifu Inyasi amesema, pamoja na mambo mengine, shule yao inakabiliwa na barabara dunia zinazoingia katika eneo la "Swaswa kwa Wasomi".







All the contents on this site are copyrighted ©.