2013-07-31 11:06:07

Boko Haram bado inaendelea kusababisha maafa nchini Nigeria


Kikundi cha Kigaidi cha Boko Haram, tarehe 29 Julai 2013 kimefanya shambulizi kwenye Kitongoji cha Sabon Gari na kusababisha vifo vya watu 12, licha ya kampeni kubwa inayoendeshwa na Serikali kutaka kukidhibiti Kikundi cha Boko Haram katika maeneo ya Kaskazini mwa Nigeria.

Taarifa ya vyombo vya habari kutoka Nigeria inabainisha kwamba, watu 40 wanaotuhumiwa kuhusika na shambulizi hili tayari wamekwishakamatwa. Wananchi wametakiwa kuchukua tahadhari kubwa kwani wanaweza kushambuliwa wakati wowote.

Katika mahojiano na Radio Vatican, Kardinali John Onayekan wa Jimbo kuu la Abuja, Nigeria anasema, inasikitisha na kutia uchungu kuona watu wasiokuwa na hatia wanaendelea kupoteza maisha yao kwa vitendo vya kigaidi nchini Nigeria. Hii inaonesha kwamba, amani haiwezi kupatikana kwa kutunishiana misuli kati ya Serikali na Kikundi cha Boko Haram, ambacho kimekuwa kikihusika na mashambulizi ya kigaidi nchini Nigeria.

Kuna haja ya kuendeleza majadiliano ya kidini ili kuweka mikakati ya ujenzi wa Nigeria mpya inayojikita katika misingi ya haki, amani, utulivu na maendeleo endelevu. Pengine tatizo la kikundi cha Boko Haram halijapewa kipaumbele cha kutosha, ndiyo maana kinaendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu na mali zao. Serikali inapaswa kuendeleza mikakati ya ulinzi na usalama kwa ajili ya wanananchi wa Nigeria.

Kardinali Onayekan anasema kuna umuhimu pia kwa wananchi wengi nchini Nigeria kuhusishwa katika mchakato wa kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu, kwani bila amani na utulivu mambo mengi yataendelea kuharibika nchini Nigeria.







All the contents on this site are copyrighted ©.