2013-07-30 09:17:00

Wanawake wanapaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa!


Katika shida na mahangaiko ya watu kutokana na vita pamoja na kukosa makazi, kuna haja kwa Jamii kuheshimu utu wa wanawake wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kwani wanaendelea kutoa mchango mkubwa kwa Jamii zao. Licha ya umaskini wa kipato, bado ni kundi linalotoa msaada mkubwa kwa kutegemeza familia pamoja na kushiriki mchakato wa kutafuta amani na upatanisho nchini mwao.

Wanawake ni waathirika wakubwa wa vita, kinzani na migongano ya kijamii hali inayochangiwa pia na kukomaa kwa mfumo dume unaoendelea kuwanyanyasa wanawake na wasichana wengi Barani Afrika. Ni waathirika wakubwa wa umaskini wa hali na kipato, rushwa na ufisadi bila kusahau utawala mbovu. Pamoja na changamoto zote hizi, wanawake wanajikuta wakiwa na dhamana ya kuzihudumia familia zao hasa vijijini. Umefika wakati kwa wanawake Barani Afrika kuwezeshwa kwa njia ya elimu makini, uwezo wa kiuchumi pamoja na kumilikishwa ardhi na mali.
Wanawake vijijini na hata katika baadhi ya miji wanalazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji na wakati mwingine uhaba wa nishati ya umeme wa uhakika inakuwa ni kero kubwa. Ili kukabiliana na mwelekeo tenge wa maisha, mahali ambapo wanawake wanadhulumiwa na kunyanyaswa, Shirika la Masista wa Upendo wa Yesu na Maria, katika kipindi cha miaka kumi, wamekuwa mstari wa mbele kuwajengea wanawake wa Kananga uwezo wa kielimu na kiuchumi ili waweze kuzitegemeza familia zao.

Shirika hili limekuwa likitoa elimu kwa wasichana na wanawake ili kuboresha hali ya maisha yao kwa sasa na kwa siku za usoni. Inasikitisha kuona na kusikia kwamba, hata katika ulimwengu mamboleo kuna wasichana wanaolazimishwa kuolewa wakiwa na umri mdogo kabisa, yaani kati ya miaka 13 na 14, kutokana na sababu za kiuchumi na kisiasa, matokeo yake hali ya maisha inazidi kuwa ngumu.

Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Hispania, Manos Unidas limeendelea kuunga mkono jitihada za Makanisa mahalia katika kuwajengea uwezo wanawake ili kupambana na mazingira na hali yao ya maisha kwa kuwapatia ujuzi na maarifa. Lengo ni kuhakikisha kwamba, wanawake wanaheshimiwa na kuthaminiwa hata katika mfumo dume ambao kwa sasa umepitwa na wakati.







All the contents on this site are copyrighted ©.