2013-07-30 09:50:24

Vijana simameni kidete kujenga utamaduni wa haki na amani duniani


Vijana kutoka katika Baraza la Makanisa Ulimwenguni, walishiriki pia katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 huko Rio de Janeiro, Brazil, kuanzia tarehe 23 hadi tarehe 28 Julai 2013. Kauli mbiu ya Maadhimisho haya ni "basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa ni wanafunzi."

Matukio makuu ya Maadhimisho haya yalimshikirisha Baba Mtakatifu Francisko aliyewahimiza vijana kwenda kumtangaza Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Vijana kutoka Baraza la Makanisa Ulimwenguni walishiriki kikamilifu katika mijadala inayohusu mbinu mkakati wa ujenzi na uimarishaji wa misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli. Vijana walipata nafasi ya kuzungumzia changamoto mbali mbali wanazokumbana nazo katika maisha ya ujana ambayo kwa miaka ya hivi karibuni yamekuwa ni "nongwa".

Vijana kutoka Baraza la Makanisa Ulimwenguni wamekazia pamoja na mambo mengine umuhimu wa vijana kujenga utamaduni wa kuheshimiana na kuthaminiana kwa kuondokana na tabia ya ubaguzi wa rangi, hali ya kutovumiliana kiimani na badala yake wawe ni wajenzi wakuu wa misingi ya haki na amani, kwani wao wa hamu na ari ya kutaka kuishi, kumbe, vita ni kinyume cha hamu hii inayobubujika kutoka katika undani wa maisha yao.

Katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 vijana wamepata fursa ya kusikiliza katekesi za kina; wakashiriki katika Maadhimisho ya Liturujia ya Neno la Mungu na Ibada ya Misa Takatifu. Ulikuwa ni muda wa majiundo makini na fursa ya kutembelea mabanda mbali mbali ya maonesho, michezo na majadiliano.

Vijana wamechambua changamoto katika ujenzi wa haki, utunzaji bora wa mazingira, athari za myumbo wa uchumi kimataifa; vijana na haki msingi za kijamii; biashara haramu ya binadamu sanjari na changamoto ya Uinjilishaji Amerika ya Kusini. Vijana wameshiriki kikamilifu katika majiundo haya. Ni matumaini ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwamba, watajitahidi kuwa ni watangazaji hodari wa Habari Njema ya Wokovu.







All the contents on this site are copyrighted ©.