Igeni fadhila za watakatifu Joakim na Anna katika malezi ya watoto wenu!
Wakristo wa Parokia ya Mtakatifu Anna Mgange Nyika iliyoko katika Dekania ya Taita
jimbo kuu la Mombasa nchini Kenya wamesheherekea sikukuu ya somo wao kwa shangwe na
nderemo kuu hapo mwishoni Jumamosi iliyopita, 27.07.2013. Sherehe hizo zilitanguliwa
na siku tisa za kusali Novena kwa ajili ya kutayarisha mioyo ya wakristu hao ili kumuenzi
vilivyo Mama Anna somo na Msimamizi wa Parokia hiyo. Akiongoza ibada ya Misa
Takatifu ili kuadhimisha siku hiyo, Paroko Mathew Mbuthia aliwahimiza wakristu wa
Mgange Nyika kuziiga fadhila na karama za Mtakatifu Anna, Mama yake Bikira Maria kwa
kuwalea watoto na vijana wao vyema ili waweze kuisikiliza daima sauti ya Mungu kuhusu
wito wao wa dhati kama walivyofanya wazazi Joakim na Anna kwa mtoto wao Bikira Maria
ambaye hatimaye, aliweza kuupokea wito wa kuwa Mama wa Mungu na Kanisa.