2013-07-29 08:43:06

Vijana nendeni bila woga kuhudumia!


Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi ni ujumbe wa Yesu kwa kila mfuasi wake na kwamba, limekuwa ni jambo la kupendeza kuona umati mkubwa wa vijana wakishiriki katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013, changamoto ya kuhakikisha kwamba, vijana walioshiriki Maadhimisho haya wanawashirikisha na kuwaonjesha wengine uzoefu na mang'amuzi waliyokutana nayo mjini Rio de Janeiro, Brazil.

Ni sehemu ya mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko katika Ibada ya Misa Takatifu kufunga Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013. Baba Mtakatifu anawataka vijana kwenda, bila woga kuhudumia. Haya ni maneno ambayo yamejenga msingi wa mahubiri ya Baba Mtakatifu kwa umati wa vijana, Jumapili tarehe 28 Julai 2013.

Anasema, katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana wamebahatika kufanya mang'amuzi ya pamoja ya kukutana na Yesu, mwaliko kwa sasa ni kuhakikisha kwamba, uzoefu na mang'amuzi haya wanawashirikisha wengine bila ya kujibakiza na kamwe wasiwe wachoyo kwa kuwamegea wale walio karibu nao tu! Vinginevyo ni sawa na kuzimisha moto wa Injili ambao tayari umekwisha washwa mioyoni mwao.

Huu ni mwaliko wa kushirikisha mang'amuzi ya imani, kushuhudia imani na kutangaza Injili ya Kristo kama dhamana na utume ambao Kristo amelikabidhi Kanisa lake. Ni dhamana inayotekelezwa na watu makini, walio huru; watu wanaojisikia kuwa kweli ni marafiki na ndugu zake Yesu. Yesu anawatuma na anaendelea kuwasindikiza katika utekelezaji wa dhamana ya utume wa upendo.

Hapa kila mtu anashirikishwa, kwani Injili ya Kristo ni kwa ajili ya wote na wala si kwa kikundi cha wateule wachache, Injili inapaswa kuwafikia hata wale walioko pembezoni mwa Jamii, wale wanaoonekana kutojali wala kuguswa na Injili.

Baba Mtakatifu Francisko anapenda kutoa changamoto hii kwa vijana wanaotoka Amerika ya Kusini, wanaoendelea kujitoa kimasomasko kwa ajili ya shughuli za Uinjilishaji huko Amerika ya Kusini, kumkumbuka na kumwomba Mwenyeheri Josè de Achieta, mtume wa Brazil, aliyejitosa kutangaza Injili akiwa na umri wa miaka 18. Hii inaonesha kwamba, kijana ni chombo makini cha Uinjilishaji kwa kijana mwenzake.

Baba Mtakatifu anawataka vijana kuondokana na woga usiokuwa na msingi wowote kwani wanapotumwa kutangaza Injili ya Kristo, anawaongoza na kuwalinda, amewaahidi kwamba atakuwa nao siku zote hadi ukamilifu wa dahari. Yesu anawatuma kama Jumuiya na wala si kama mtu mmoja mmoja. Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia vijana uwepo wa Kanisa zima pamoja na ushirika wa watakatifu katika utume huu na kamwe wasijisikie wapweke!

Baba Mtakatifu mwishoni mwa mahubiri yake anawataka vijana kuhakikisha kwamba, maisha yao yanafanana na yale ya Kristo katika: fikira, mawazo na matendo. Maisha ya Yesu ni tunu ya kuwagawia wengine, ni maisha yanayojikita katika huduma. Ili kutangaza Injili, Mtakatifu Paulo alijifanya kuwa ni mtumwa wa wote. Uinjilishaji ni ushuhuda wa upendo wa Mungu, unaovuka mipaka ya ubinafsi na umimi, tayari kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa jirani kama alivyofanya Kristo, alipowaosha miguu wanafunzi wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.