2013-07-29 12:00:34

Kila mwamini anaalikwa kuwa mtakatifu!


Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa vijana katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani huko Rio de Janeiro, Brazil ni mzito kweli. Maana ya utakatifu si muonekano wa nje bali ni badiliko la ndani, ni toba na wongofu wa ndani; ni upya uliofichika katika nafsi za vijana na uthabiti wa maisha yao machanga ya Ushuhuda na ya Kikristu katika dunia hii geu geu.

Hii itawapa moyo sana vijana ambao katika jicho la wazee walionekana wamechafua "utakatifu" wao kwa kunywa Coca Cola, kuzama kati I pads zao au kwenye matamasha ya muziki.

Haya ni mang’amuzi ya Padre Beno Michael Kikudo kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaam, anapojaribu kuwashirikisha wana ukoo wenzake kuhusu changamoto za utakatifu wa maisha, kama ulivyofafanuliwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipokuwa anakutana na vijana nchini Brazil.

Vijana waliona utakatifu kwao ni kama “msamiati wa Kichina au kitu kisichowezekana kuishika wala kumwilishwa katika uhalisia wa maisha. Vijana walidhani kwamba, utakatifu ni maisha ya kufikirika na kusadikika waliyoishi watu wa kale. Vijana waliona maisha yao kama wasindikizaji tu wa kundi jingine dogo linalotafuta utakatifu na hao kwa nasibu wamesalia katika nyumba za kitawa na maparokiani

Hatari ya kuacha na kuendeleza muono wa utakatifu katika dhana ya maisha magumu, yasiyopendeza na ushahidi mkali wa kumwaga damu tu - hatari yake ni kugandisha hamu ya kuwa watatifu katika nyumba za watawa na maghorofa ya makasisi.

Tuombe Mungu vijana wang'amue kweli kile ambacho Baba Mtakatifu Francisko alikusudia kusema kwao. Yaani, waone utakatifu katika jicho na mwanga mpya kama Bartimayo kipofu wa Yeriko (Marko 10:51) - "Mwalimu naomba nipate kuona tena.."








All the contents on this site are copyrighted ©.