Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili tarehe 28 Julai 2013 alikutana na vijana waliokuwa
wanajitolea kutoa huduma, akawashukuru kwa moyo wa ukarimu na uungwana waliouonesha
kwa vijana wenzao wakati wa Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka
2013 huko Rio de Janeiro, Brazil. Baba Mtakatifu anasema, ni kheri kutoa kuliko kupokea
kama yanavyosema Maandiko Matakatifu.
Katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana,
wameshiriki kwa njia ya huduma, kama alivyofanya Yohane Mbatizaji kabla Yesu kuanza
maisha ya hadhara, akamwandalia mapito. Kwa upande wa vijana waliokuwa wanajitolea,
wamekuwa ni chombo cha maandalizi kwa ajili ya vijana kuweza kukutana na Yesu.
Baba
Mtakatifu anawakumbusha kwamba, Mwenyezi Mungu ana mpango na kila mmoja wao, jambo
la msingi ni kugundua mpango wa Mungu katika hija ya maisha yao na hatimaye, kuufanyia
kazi. Mwenyezi Mungu anawaalika wote kuwa ni watakatifu na kila mmoja anaweza kuufikia
utakatifu wa maisha kwa njia tofauti. Baadhi ya waamini wanaalikwa kuwa watakatifu
kwa njia ya Sakramenti ya Ndoa Takatifu, ili kujenga familia na kwamba, ndoa ni zawadi
kubwa ambayo Mwenyezi Mungu anawakarimia waja wake ili kushiriki katika kazi ya Uumbaji
inayowawajibisha.
Baba Mtakatifu anaonya kwamba, kuna baadhi ya watu wanadhani
kwamba, ndoa ni mambo yaliyopitwa na wakati, lakini kwa waamini hii ni dhamana endelevu,
changamoto ya kuwa na maamuzi thabiti yanayowawajibisha katika Kanisa na Jamii inayowazunguka.
Baba
Mtakatifu anasema kwa wale wanaoamua kuchagua wito wa Upadre, wanapaswa kujitosa kimasomaso
bila ya kujibakiza, wakipenda na kutenda kama Yesu mchungaji mwema. Baadhi ya waamini
wanaitwa pia kuwa ni watawa, ili kujitoa kwa ajili ya sala na sadaka ya maisha yao
kwa ajili ya mafao ya wengi, katika medani mbali mbali za maisha, lakini zaidi kwa
maskini na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Baba Mtakatifu amewakumbusha
kwamba, hata yeye alisikia wito wa kuwa ni Mtawa na Padre alipokuwa na umri wa miaka
17, changamoto kwa vijana kutokuwa na woga wa kusikiliza na kutekeleza kile ambacho
Mwenyezi Mungu anataka kutoka kwao. Ni vyema kukubali mpango wa Mungu katika maisha
yao, kwani Mungu ni chemchemi ya furaha ya kweli.
Baba Mtakatifu Francisko
amehitimisha hotuba yake kwa vijana waliokuwa wanajitolea kwa kuwataka kujiuliza swali
la msingi, Je, Mwenyezi Mungu anataka nini katika maisha yao! Je, ni njia ipi wanayopaswa
kuifuata ili kufikia lengo la maisha na wito wao!