Fumbo la Msalaba ni kielelezo cha upendo na huruma ya Mungu kwa binadamu!
Njia ya Msalaba ni kati ya matukio makuu yanayopamba Maadhimisho ya Siku ya Vijana
Duniani, tangu mwaka 1984, Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alipowakabidhi vijana Msalaba,
ambao umetembelea Mabara yote. Hakuna anayeweza kugusa Msalaba wa Kristo bila kuacha
sehemu ya maisha yake na kupokea neema kutoka kwa Kristo.
Ni maneno ya Baba
Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Njia ya Msalaba kwenye ufuko wa Copacabana,
kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013. Baba Mtakatifu
anawauliza vijana wa Brazil baada ya kutembeza Msalaba huu kwa takribani miaka miwili,
ni mambo yepi ambayo wameacha chini ya Msalaba? Baba Mtakatifu anaendelea kuwauliza
vijana wenyewe ni mambo yepi ambayo Kristo amewaachia wakati walipokuwa wanautembeza
Msalaba huo? Mwishoni, Baba Mtakatifu anawauliza vijana maana ya Msalaba katika maisha!
Baba
Mtakatifu anasema, Msalaba unatisha, kama ilivyojionesha hata kwa Mitume wa Yesu,
waliotaka kukimbia madhulumu ya Nerone; Petro kwa mshangao mkubwa akakutana na Yesu
njiani akielekea mjini Roma ili aweze kusulubishwa mara ya pili; hapo ndipo Mtume
Petro alipoishiwa nguvu, akapiga moyo konde na kufuata nyayo za Kristo, kiasi hata
cha kuyamimina maisha yake juu ya Msalaba kwa kutambua kwamba, Yesu alikuwa amempenda
upeo!
Baba Mtakatifu anasema, kwa njia ya Msalaba, Yesu anajiunga na wale wote
wanaodhulumiwa na kuteswa; watu ambao hawana tena nguvu ya kupiga kelele; hasa watu
wasiokuwa na hatia wala ulinzi madhubuti; familia zinazokabiliana na hali ngumu ya
maisha; wale wanaolia na kuomboleza kwa kuondokewa na wapendwa wao katika maisha;
wanaowalilia watoto wao waliotumbukia katika matumizi haramu ya dawa za kulevya.
Kwa
njia ya Fumbo la Msalaba, Yesu anaungana na mamillioni ya watu wanaoteseka kutokana
na baa la njaa wakati ambapo kuna sehemu nyingine za dunia wanakula na kusaza! Anajiunga
na wale wanaoteswa na kudhulumiwa kutokana na imani, mawazo na rangi ya ngozi. Yesu
anaendelea kujiunga na umati mkubwa wa vijana uliopoteza dira, mwelekeo na matumaini
ya maisha kutokana na wanasiasa wanaowaongoza kuelemewa mno na ubainfsi, rushwa na
ufisadi.
Baba Mtakatifu anaendelea kuwaambia vijana kwamba, Yesu anaendelea
kuungana kwa njia ya Fumbo la Msalaba na waamini ambao wamepoteza imani yao kwa Mungu
na Kanisa kutokana na kashfa na utepetevu wa imani ulioneshwa na watumishi wa Injili.
Yesu anayapokea yote haya kwa mikono miwili na kujitwika mabegani mwake pamoja na
Misalaba ya wafuasi wake, tayari kuwaambia, jipeni moyo kwani yuko pamoja nao na kwamba,
ameshinda dhambi na mauti na yuko kati yao ili kuweza kuwakirimia matumaini na maisha
tele!
Baba Mtakatifu Francisko anawauliza vijana ni mambo yepi ambayo Fumbo
la Msalaba limewaachia baada ya kuuona na kuugusa Msalaba ulipokuwa unatembezwa mitaani
na kwenye viunga vyao vya maisha? Jibu makini linajikita katika upendo wa Mungu kwa
binadamu wote.
Ni upendo ambao unapenya katika mapungufu na dhambi za mwanadamu
kiasi cha kumkirimia msamaha; upendo unaopenya katika taabu na mahangaiko ya binadamu
kiasi cha kumjalia nguvu ya kuweza kuyabeba na kuyavumilia; upendo umegusa hata mauti,
na kuyashinda na hatimaye kumkirimia mwanadamu maisha ya uzima wa milele.
Yesu
anawajalia wafuasi wake matumaini na maisha tele! Amegeuza ile kashfa ya Msalaba ulioonekana
kuwa ni chombo cha chuki na uhasama, anguko na kifo, kuwa ni alama ya ushindi na maisha.
Hakuna Msalaba mdogo wala mkubwa katika maisha, bali ni uwepo endelevu wa Kristo anayetaka
kushiriki na kuwamegea wafuasi wake maisha na uzima wa milele.
Baba Mtakatifu
anasema, Msalaba ni mwaliko wa Kristo kwa wafuasi wake ili waweze kuguswa na upendo
wa dhati unaobubujika kutoka katika Fumbo la Msalaba. Ni changamoto ya kuendelea kumtumainia
Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma na mapendo; hasa zaidi kwa wale wanaoteseka; watu
wanaohitaji msaada; ni jukumu la kila mwamini kujitoa katika ubinafsi wake ili kuwaendelea
na kuwanyooshea mikono tayari kuwasaidia wengine.
Baba Mtakatifu anawaambia
vijana kwamba, hata wao wanaweza kuwa kama Pilato anayeelemewa na woga kiasi cha kushindwa
kuokoa maisha ya Yesu dhidi ya kifo, anajiondoa kwenye hatia hii kwa kunawa mikono
yake! Fumbo la Msalaba ni mwaliko kwa kila mwamini kuwa kama Simoni wa Kirene, aliyemsaidia
Yesu kubeba Msalaba, kama ilivyokuwa kwa Bikira Maria na kwa wanawake wengine watakatifu,
waliopiga moyo konde, wakaifuata ile njia ya uchungu wakiwa wamesheheni upendo na
huruma hadi chini ya Msalaba.
Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha tafakari
yake wakati wa Njia ya Msalaba kwenye ufuko wa Copacabana kama sehemu ya Maadhimisho
ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa kumuuliza kila kijana, anajisikia kuwa ni nani
katika Njia hii ya Msalaba: Pilato, Simoni wa Kirene au Bikira Maria?