Kila kijana anaweza kuwa ni shahidi wa upendo na ujasiri wa Injili ya Kristo ili kupeleka
mwanga katika ulimwengu mamboleo!
Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwaalika vijana kujenga utamaduni wa kumsikiliza
Kristo kwa umakini mkubwa, ili waweze kumpokea na kumkaribisha katika hija ya maisha
ya ujana wao. Yesu ni Neno wa Mungu aliyefanyika mwili kwa njia ya Roho Mtakatifu
anawaletea mabadiliko na anawaangazia katika mapito yao kwa siku za usoni.
Roho
Mtakatifu anawawezesha waamini kukuza ndani mwao fadhila ya matumaini ili waweze
kutembea kwa furaha! Baba Mtakatifu Francisko ameyasema haya wakati wa sehemu ya pili
ya tafakari yake kwa ajili ya kuwakaribisha vijana kwenye Maadhimisho ya Siku ya 28
ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.
Baba Mtakatifu anawataka vijana katika safari
ya maisha yao ya ujana kutoa kipaumbele cha pekee kwa imani, matumaini na mapendo,
ili kujenga maisha yao katika mwamba thabiti na hivyo kutembea kwa furaha sanjari
na kukutana na marafiki wengine wanaofanya hija pamoja nao! Fadhila hizi zinapata
chimbuko lake kutoka kwa Kristo, kiasi kwamba, vijana wanaweza kuuangalia ukweli wa
maisha kwa ujasiri mkubwa, kwani Yesu Kristo ni rafiki na mwenza anayeaminika.
Huu
ni mwaliko kwa vijana kumpokea na kumruhusu Kristo kuwa kweli ni dira na mwongozo
wa maisha yao. Kuna vijana wengi wanaotaka kujenga maisha na kuwa na furaha inayojikita
katika mali na madaraka, lakini haya ni mambo ya mpito, ikiwa kama Kristo atakuwa
ni nguzo ya maisha ya kijana, kamwe kijana huyu hataweza kudanganyika.
Imani
inamwezesha mwamini kuona mabadiliko na kuwa na usalama, nguvu na matumaini. Bila
ya uwepo wa Mungu, maisha ya mwanadamu ni ubatili mtupu! Baba Mtakatifu anawaambia
vijana katika sakafu ya mioyo yao kuna matunda ya Roho Mtakatifu ambayo ni: upendo,
furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole na kiasi. Mwamini akimruhusu
Yesu kutenda kazi ndani mwake atafanikiwa kuwa ni shahidi amini wa Kristo.
Baba
Mtakatifu Francisko anasema, katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Siku ya Vijana
Duniani inakuwa ni zawadi kubwa kwa vijana ili kuweza kumkaribia zaidi Kristo, ili
kuwa kweli ni wanafunzi na wamissionari wake, huku wakiendelea kutoa nafasi kwa Kristo
aweze kuwaletea mabadiliko ya kweli katika maisha!
Kwa msisitizo mkubwa, Baba
Mtakatifu anawaalika vijana kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo, kwa njia ya kumsikiliza
kwa makini, kumpokea katika Sakramenti za Kanisa, lakini kwa namna ya pekee, katika
Sakramenti ya Upatanisho, ili aweze kuwaganga majeraha ya dhambi kwa njia ya huruma
yake. Kamwe vijana wasiogope kumwomba Mungu msamaha wa mapungufu ya maisha yao, kwani
Mwenyezi Mungu daima yuko tayari kuwasamehe dhambi zao, kwani anawapenda na mwingi
wa huruma.
Baba Mtakatifu anawaalika vijana kumpokea Kristo katika Sakramenti
ya Ekaristi Takatifu, inayoonesha uwamo wake endelevu katika Maumbo ya Mkate na Divai;
Sadaka ya Mapendo na chemchemi ya urafiki wa kina utakaoendelea kuyatajirisha maisha
ya vijana kwa njia ya ushuhuda wa imani; watafundishwa lugha ya upendo, wema na huduma.
Kila kijana anaweza kuwa ni shahidi wa upendo na ujasiri wa Injili ya Kristo ili kupeleka
mwanga katika ulimwengu mamboleo.
Mwishoni Baba Mtakatifu anasema, inapendeza
kukaa hapa kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo anayewakirimia: imani, matumaini
na mapendo. Anawaalika vijana kuwa kweli ni Wamissionaro wa Kristo kwa kukubali mwaliko
na wito wake, ili waweze kumpenda na kumfanya Kristo apendeke zaidi. Yesu anawasubiri
na kwamba, ana matumaini makubwa kwa vijana!