2013-07-25 10:14:42

Kanisa ni kijana kutokana na ujana wa vijana wenyewe! Maajabu ya Mungu!


Mheshimiwa Padre Raymond Saba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani anasema, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania limetuma ujumbe "mnene" kwenye Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani huko Rio de Janeiro, Brazil. RealAudioMP3

Padre Saba katika mahojiano na Radio Vatican anasema kwamba, vijana wanapaswa kupambua dhamana na wajibu wao ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla kwamba, wao ni nguzo, jeuri na mboni ya jicho la Kanisa. Vijana wanapaswa kuwa ni chumvi na nuru ya ulimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao adili na manyofu. Ujana ni "nongwa", lakini katika ujana kuna mang'amuzi makubwa, nguvu nyingi zinazopaswa kutumia vyema kwa ajili ya mafao na maendeleo ya wengi kiroho na kimwili na wala si kwa ajili ya kubomoa! Ujana ni kipindi kilichojaa ubunifu, unaoweza kutumika pia katika azma ya Uinjilishaji wa kina.

Vijana wautumie ujana wao kuwashirikisha na kushirikishana tunu msingi za maisha ya Kiinjili; wajiimarishe na kuwaimarisha vijana wenzao katika misingi ya imani, maadili na utu wema. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alipenda kusema kwamba, Kanisa ni kijana kutokana na ujana wa vijana wenyewe anasema Padre Saba kwamba, haya ndiyo maajabu ya Mungu kwa waja wake.

Vijana wanahamasishwa kuona ari na nguvu iliyoko ndani mwao kwa njia ya ushuhuda wa maisha. Kanisa ambalo limejengwa kutokana na msingi thabiti wa mateso, kifo na ufufuko wa Kristo litaendelea kubaki ni kijana. Vijana na ujana wao ni tunu muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa.

Papa Francisko anataka kuwaimarisha vijana, ili nao kwa wakati ufaao waweze kuwaimarisha na kuwainjilisha vijana wenzao, kwani wanatumwa kwenda ulimwenguni kote kuwafanya mataifa yote kuwa ni wanafunzi, kauli mbiu inayoongoza Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.