2013-07-24 16:07:19

Picha ya Bikira Maria wa Aparecida iwe ni kielelezo cha mateso na mahangaiko ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii!


Kardinali Damasceno Assis, Askofu mkuu wa Aparecida katika hotuba yake ya utangulizi kabla ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko, hapo tarehe 24 Julai 2013, ameelezea historia fupi ya Madhabahu ya Bikira Maria wa Aparecida, tangu mwaka 1717.

Mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia wamefika na kutembelea Madhabahu haya, wakiwa wanaongoza na matumaini. Hija ya Baba Mtakatifu mahali hapo ni fursa ya kuwaimarisha ndugu zake katika ukweli wa imani na upendo katika hija ya utakatifu wa maisha.

Madhabahu ya Bikira Maria wa Aparecida ni kielelezo na utambulisho muhimu wa Brazil, ndiyo maana Baba Mtakatifu amependa kuweka Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Aparecida, ili awaimarishe vijana katika imani, matumaini na mapendo thabiti kwa Yesu, daima wakiwa tayari kumwilisha ujumbe wa Yesu, unaowachangamotisha kwenda ulimwenguni kote kuwafanya mataifa yote kuwa ni wanafunzi.

Madhabahu haya yamekwisha wapokea Mwenyeheri Yohane Paulo II, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, na leo hii, Papa Francisko. Kardinali Damasceno Assis amemzawadia Baba Mtakatifu Picha ya Bikira Maria wa Aparecida, inayoonesha mateso na mahangaiko ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, hasa wananchi wa Brazil ambao wana asili ya kiafrika. Hii ni Jamii ambayo imeshuhudia pia ubaguzi na nyanyaso katika maisha yao.

Hii ni changamoto kwa Kanisa Katoliki nchini Brazil kujikita katika dhamana ya Uinjilishaji mpya, kwa kuonesha mshikamano na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; wakiwa huru, waweze kuhudumia kwa ukamilifu zaidi. Kanisa nchini Brazil linamtakia kheri, baraka na mafanikio katika maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Wanamwombea ili aweze kuwa shahidi mwaminifu katika kutangaza na kushuhudia kweli za Kiinjili; imara katika imani anapokumbana na changamoto za maisha, daima akitegemea ulinzi na usimamizi wa Mwenyezi Mungu na maombezi ya Bikira Maria wa Aparecida.







All the contents on this site are copyrighted ©.