2013-07-24 08:15:06

Hali ya wakimbizi eneo la Maziwa Makuu bado si shwari!


Askofu mkuu Paul Ruzoka, Mwenyekiti wa Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano na maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, Tanzania ambayo imekuwa ikitoa hifadhi kwa wakimbizi kutoka sehemu mbali mbali za nchi za Maziwa Makuu inakabiliwa na changamoto kadhaa. Ukweli ni kwamba, kwa sasa kuna wakimbizi wachache wanaoishi nchini Tanzania. RealAudioMP3

Lakini hapa kinachoangaliwa anasema Askofu mkuu Ruzoka, si idadi ya watu, bali kila mtu anapaswa kuangaliwa kama mtu binafsi anayetafuta hifadhi, usalama na nafuu ya maisha kutokana na sababu mbali mbali nchini mwake zinazomlazimisha kuyahama makazi yake. Tangu kunako mwaka 1959, Tanzania imekuwa ikitoa hifadhi kwa wakimbizi kutoka Rwanda na kunako mwaka 1972 ikaanza pia kupokea wakimbizi kutoka Burundi nab ado kuna idadi ndogo ya wakimbizi wanaoishi ndani ya mipaka ya Tanzania.

Kumekuwepo na mchakato kwa wakimbizi kuamua kurudi makwao au kubaki Tanzania na kupewa uraia wa Tanzania. Hofu bado imetanda kwa wale wakimbizi waliojiandikisha kuomba uraia wa Tanzania, kwani hadi sasa bado hawajapata jibu muafaka na hivyo hawana habari kwa kile kinachoendelea kwa sasa. Kigoma kuna wakimbizi kutoka DRC wanaoishi kwenye Kambi ya wakimbizi ya Nyalugusu, wote hawa wanatafuta hifadhi na usalama wa maisha yao na kwamba, Serikali ya Tanzania inaendelea kulishughulikia tatizo hili.

Kanisa limekuwa mstari wa mbele kuwahudumia wakimbizi kwa hali na mali pamoja na kuwapatia huduma za kiroho kwa wale wakimbizi wanaoishi Tabora na Kigoma. Tangu mwaka 1973 maeneo yao yamekuwa ni Parokia, utume ambao unaendelezwa kwa sasa.

Askofu mkuu Ruzoka anasema, hali ya wakimbizi kwenye nchi za Maziwa Makuu bado ni tete kutokana na mgogoro wa kisiasa na vita inayoendelea huko Mashariki mwa DRC kati ya Jeshi la Serikali na M23. Hivi karibuni, nchi za SADC zimeamua kupeleka vikosi vya ulinzi na usalama ili kusaidia mchakato wa kuleta amani nchini DRC. Migogoro ya kisiasa na vita huko DRC ni mambo ambayo yataendelea kuzalisha wimbi kubwa la wakimbizi.

Askofu mkuu Paul Ruzoka ambaye pia ni mjumbe wa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi anasema, katika mkutano wao uliohitimishwa hivi karibuni mjini Vatican, Baba Mtakatifu Francisko aliwakumbusha kwamba, suala la wakimbizi na wahamiaji ni tete na kwamba, Kanisa halina budi kuendelea kujishughulisha zaidi na watu wanaoishi katika mazingira hatarishi: kwa kuwatia moyo, kuwahudumia pamoja na kuwajengea misingi ya: haki, amani, upatanisho na utulivu.

Kanisa liendeshe shughuli zake kwa njia ya ushawishi kwa kuhakikisha kwamba, Serikali inawajali raia wake na wale wanakimbilia usalama na amani katika mipaka yake, kwani hakuna maendeleo ya kweli na endelevu pasi ya haki na amani.








All the contents on this site are copyrighted ©.