2013-07-23 10:51:03

Vijana msiwe ni bendera kufuata upepo, mtalizwa na wajanja!


Padre Beno Michael Kikudo kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaam anawaambia vijana wanaohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 huko Rio de Janeiro kwamba, hili ni tukio muhimu sana katika maisha yao ya kiroho na ustawi wa maendeleo yaokwa siku za usoni. Hiki si kipindi cha utalii na kuvinjari mazingira ya Brazil ambayo inasifika sana kwa kutandaza kabumbu duniani na yenye vivutio vingi vya kitalii! RealAudioMP3

Vijana watambue kwamba, wamepewa fursa na Mama Kanisa ya kufanya hija ya maisha yao ya kiroho, inayowawezesha kukutana na vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia; changamoto ya kutuliza mawazo, maneno na matendo yao, ili waweze kufaidika na yale ambayo Mama Kanisa amewaandalia. Vijana wawe makini katika sala, katekesi, maadhimisho ya Ibada mbali mbali, ili kufanikisha malengo ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, wakiwa tayari kuzijibia changamoto za ujana katika maisha yao ya kila siku.

Padre Kikudo anasema, vijana wa kitanzania maarufu kama "vijana wa bongo country" wanakabiliana na changamoto zile zile kama ilivyo kwa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Kwa vijana ambao hawakupata fursa ya kwenda Brazil, wahamasike kuungana na vijana wenzao kadiri ya nafasi na fursa zilizopo ili wasipitwe kamwe na yale yanayojiri katika Maadhimisho haya.

Kila kijana anachangamotishwa na Mama Kanisa kutambua dhamana na wajibu wake ndani ya Jamii, tayari kuutekeleza kwa moyo mkuu na ari kubwa zaidi. Kijana anapaswa kuwa na msimamo thabiti katika maisha na kamwe asiwe ni bendera kufuata upepo kwani anaweza "kulizwa" na wajanja katika maisha!







All the contents on this site are copyrighted ©.