2013-07-23 08:29:12

Brazil inatambua mchango wa Papa Francisko katika kutetea haki jamii!


Rais Dilma Rouseff wa Brazil, amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko, Khalifa wa kwanza wa Mtakatifu Petro kutoka Amerika ya Kusini anayetembelea Brazil katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013. Vijana wa Brazil wapatao millioni 50 wanaungana na vijana wengine kutoka sehemu mbali mbali za dunia kumpokea Baba Mtakatifu kwa moyo wa ukarimu.

Brazil inamtambua Papa kuwa ni kiongozi wa kiroho, mtu makini katika masuala yanayogusa haki jamii na adui mkubwa wa ubaguzi kati ya watu na utandawazi unaowafanya watu kutoguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wengine. Ni kiongozi anayependa kutetea wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kama inavyojionesha katika jina alilolichagua yaani Francisko.

Rais Dilma Rouseff anasema, Brazil imepiga hatua kubwa ya maendeleo, lakini bado kuna mambo mengi yanayopaswa kuboreshwa. Njaa na kiu ya haki ni kati ya mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza. Hivi ndivyo ilivyojionesha katika maandamano na vurugu za kisiasa zilizojitokeza hivi karibuni.

Serikali kwa kuendelea kushirikiana na Kanisa nchini Brazil kwa pamoja wanapania kuvuka vikwazo vya myumbo wa uchumi kimataifa kwa kutoa nafuu ya maisha kwa maelfu ya watu wasiokuwa na fursa za ajira na maskini. Lengo ni kuondokana na woga usiokuwa na msingi pamoja na makosa ya jinai.

Brazil ni nchi ya watu wenye imani zao, lakini wanakabiliana na changamoto nyingi kama inavyojionesha nchini humo, kwani kumekuwepo na maandamano kupinga sera na mikakati ya Serikali; yote haya yanaonesha utashi wa wananchi wa Brazil kutaka kuwa na maisha bora zaidi. Vijana wa Brazil wamepania kufanya maboresho ya kina katika maisha yao, jambo muhimu sana hata katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

Rais Dilma Roussef anasema vijana wana ari, moyo na furaha; wanaonesha ujasiri na mwamko wa kutaka kupata fursa ya kugundua tunu msingi za maisha. Ni matumaini yake kwamba, Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani nchini Brazil yataleta matunda yanayokusudiwa kwa vijana nchini Brazil na kutoka sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.