2013-07-23 09:45:07

Biashara haramu ya binadamu ni uvunjifu wa msingi ya utu na heshima ya binadamu


Viongozi wa Makanisa nchini Ufilippini wanaendelea kushikamana kupinga biashara haramu ya binadamu inayoendelea kushamiri nchini humo siku hadi siku. Wanaitaka Serikali ya Ufilippini pamoja na Serikali za nchi nyingi za Kiasia, kuhakikisha kwamba, zinachukua hatua za kisheria dhidi ya biashara haramu ya binadamu, hali ambayo inaendelea kusababisha uvunjifu wa misingi ya utu na heshima ya binadamu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. RealAudioMP3

Hayo yamebainishwa hivi karibuni na Askofu msaidizi Broderick Pabillo wa Jimbo kuu la Manila. Anasema, biashara haramu ya binadamu ni tatizo linaloendelea kuota mizizi nchini humo, kumbe, kuna haja kwa Jamii ikisaidiana na Serikali kuweka mikakati ya kupambana na biashara hii inayowatumbukiza watoto na wasichana katika utumwa mamboleo. Makanisa hayawezi kukaa kimya huku utu na heshima ya binadamu vikiendelea kudhalilishwa na watu wachache wenye uchu wa mali na utajiri wa haraka haraka kwa kutumia mgongo wa wanyonge ndani ya Jamii.

Biashara haramu ya binadamu ni matokeo ya umaskini, rushwa na uvunjaji wa sheria unaofanywa na baadhi ya watu kwa kushirikiana na vyombo vya usalama kwa ajili ya mafao ya binafsi. Ni biashara ambato inawatumbukiza watoto na wasichana katika biashara ya ukahaba na kwamba, Serikali bado inaendelea kulifumbia macho tatizo hili licha ya taarifa za Jumuiya ya Kimataifa iliyochapishwa kunako mwaka 2012 kuonesha kwamba, waathirika wa biashara hii hawana hifadhi yoyote ile!

Wahusika wa biashara haramu ya binadamu wanaendelea kula “kuku kwa mrija” wakati ambapo utu na heshima ya binadamu inadhalilishwa na kutezwa. Wahusika wameshindwa kufikishwa kwenye vyombo vya kisheria ili sheria iweze kuchukua mkondo wake! Biashara haramu ya binadamu inalenga pia kutoa ajira kwa ujira mdogo kwa makampuni makubwa ya kimataifa yanayoendelea kuwekeza Barani Asia, Mashariki ya Kati, Ulaya na Marekani.

Takwimu zinaonesha kwamba, idadi ya wananchi kutoka nchini Ufilippini imefikia walau millioni kumi! Rais Benigno Aquino wa Ufilippini, ameipokea changamoto hii kwa mwelekeo chanya na kuahidi kwamba ataifanyia kazi, ili kudhibiti biashara haramu ya binadamu.








All the contents on this site are copyrighted ©.