2013-07-22 08:18:57

Masista wa Ivrea waanza Maadhimisho ya Jubilee za maisha ya kitawa!


Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili ya Kristo ndiye atakayeisalimisha. Huu ni muhtsari wa ujumbe wa Yesu kwa wafuasi wake wa nyakati zote. Mtu kuiangamiza nafsi yake kwa ajili ya Yesu kuna maana kuu mbili: kuiungamana imani au kusimama kidete kutetea ukweli! RealAudioMP3

Mashahidi na waungama imani ni wale ambao wameyamimina maisha yao kwa ajili ya Yesu Kristo. Katika kipindi cha miaka elfu mbili ya Ukristo kuna Wakristo wengi waliopoteza maisha yao ikilinganishwa na idadi ya Wakristo wa Kanisa la Mwanzo. Ni mashahidi waliothubutu kujitoa kimasomaso ili kuendelea kuwa waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake.

Ni tafakari iliyotolewa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko na kuendelea kusema kwamba, Mashahidi wa Injili wanaojionesha kila siku ya maisha, wakati wakitekeleza dhamana na wajibu wao kwa Kanisa, Familia na Jamii inayowazunguka.

Hawa ni Makleri, Watawa, Wazazi na Walezi pamoja na vijana. Ni watu wanaoonesha sadaka ya maisha yao kwa Kristo na Kanisa lake; wanajitahidi kurithisha imani na mafao kwa watoto wao ni vijana wanaojitoa kwa ajili ya kuwasaidia wahitaji zaidi.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, hata hawa ni mashahidi wa Kristo katika uhalisia wa maisha ya kila siku. Kuna Wakristo na watu wengine katika Jamii ambao wameyamimina maisha yao kwa ajili ya kulinda na kutetea ukweli, kwani Kristo mwenyewe amesema, Yeye ndiye ukweli na uzima.

Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Shirika la Masista wa Upendo wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili la Ivrea, linawaalika watawa wake kuwa waaminifu kwa wito na maisha yao ya kitawa, kwa kutambua kwamba, Mwenyezi Mungu daima ni mwaminifu katika ahadi zake.

Kutokana na ukweli huu, Shirika hili linawasherehekea watawa wake waliotimiza miaka 15, 25 na 35 ya maisha ya kitawa, kwa kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani, huku wakiyaelekeza macho yao kwa Bikira Maria, Mama aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kutekeleza mpango wa Mungu katika maisha yake.

Mheshimiwa Sr. Palma Porro, Mama Mkuu wa Shirika la Masista wa Upendo wa Bikira Maria Mkingiwa dhambi ya Asili la Ivrea anasema kwamba, kuanzia tarehe 21 hadi 28 Julai 2013, Masista 23 kutoka sehemu mbali mbali za dunia watakusanyika mjini Roma ili kujinoa katika tasaufi ya maisha yao ya kiroho. Kuanzia tarehe 29 Julai hadi tarehe 16 Agosti 2013 watakuwa Andrate, Kaskazini mwa Italia kushiriki katika kozi ya majiundo endelevu na kilele cha Jubilee hizi ni hapo tarehe 15 Agosti 2013, Siku kuu ya Bikira Maria Kupalizwa mbinguni.

Maadhimisho haya yatafanyika kwenye Kanisa la Bikira Maria wa Miujiza, Jimboni Ivrea. Huu utakuwa ni muda muafaka wa kusali, kutafakari kwa kina Neno la Mungu, pamoja na kushirikishana, furaha, majonzi na mang’amuzi ya maisha ya kitawa.

Masista wa Upendo wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili wa Ivrea, watakuwa wanasindikizwa na Mwenyeheri Mama Antonia Maria Verna, mwanamke wa shoka, aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani.








All the contents on this site are copyrighted ©.