2013-07-22 08:57:58

Caritas Hong Kong katika huduma ya watu: kiroho na kimwili!


Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki Jimbo kuu la Hong Kong, hivi karibuni limeadhimisha kumbu kumbu ya miaka 60 tangu lilipozinduliwa na hivyo kuwa kwelini kitovu cha majiundo na mikakati ya maendeleo endelevu. Caritas Hong Kong ni kati ya Mashirika makubwa ya Misaada ya Kanisa Katoliki katika ngazi ya Kijimbo. RealAudioMP3

Lina jumla ya wanachama elfu kumi wanaojitolea sehemu mbali mbali Barani Asia na kwamba, lina endesha miradi mikubwa nchini Japan, India, Vietnam, New Zealand, Australia na China.

Ni maneno ya Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, baada ya kurejea mjini Vatican kutoka Hong Kong alikokuwa anahudhuria Maadhimisho ya Miaka 60 ya Caritas Hong Kong. Akiwa nchini humo, aliwasilisha pia salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko, anayetambua na kuthamini uwepo wa Kanisa Katoliki Barani Asia na kwa namna ya pekee kabisa nchini China. Hii inaonesha kwamba, Mama Kanisa anawapenda watoto wake wote bila ubaguzi wa aina yoyote ile!

Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 60 ya Caritas Hong Kong yalihudhuriwa na na wawakilishi 700 kutoka Majimbo mbali mbali Barani Asia. Ilikuwa ni nafasi kwa Kardinali Robert Sarah kuweza kujionea mwenyewe utume unaotekelezwa na Caritas Hong kong, ambayo inendelea kuwa ni mfano bora wa kuigwa katika huduma na majitoleo kwa watu wenye mahangaiko mbali mbali.

Hapa pamekuwa ni mahali pa majadiliano ya kidini na kiekumene katika mchakato wa kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Caritas Hong Kong imeonesha ukomavu wa hali ya juu kwa kushirikiana taasisi mbali mbali katika kuwahudumia watu: kiroho na kimwili.

Kardinali Sarah anasema kwamba, Caritas Hong Kong kwa sasa imeajiri wafanyakazi 5,500. Kuna watu wa kujitolea wapatao 10, 000. Huu ni ushuhuda unaoonesha jinsi ambavyo Caritas Hong Kong imejiingiza katika maisha na mateso ya watu, kiasi kwamba, kimekuwa ni chombo cha huduma ya: huruma, upendo na mshikamano. Caritas kwa miaka ya hivi karibuni imeanza kujielekeza zaidi katika majiundo makini na endelevu kwa wananchi wa Bara la Asia.

Kwa sasa Caritas imejiwekea mkakati wa kutaka kuanza ujenzi wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Barani Asia, kitakachochangia kwa hali na mali katika majiundo ya mtu mzima: kiroho na kimwili na huduma ya upendo.

Mama Kanisa ameendelea kufanya hija na Waamini wa Kanisa Katoliki nchini China kwa kutambua fursa, matatizo na changamoto mbali mbali wanazokabiliana nazo katika kumshuhudia Kristo na Kanisa lake. Kanisa linawatambua watoto wake na kuwakumbatia wote kwa upendo wa kimama!








All the contents on this site are copyrighted ©.