Mwaka wa Imani: Wanovisi na walelewa iweni watu wa imani, matumaini na mapendo!
Rev. Dr. Sr. Sabina Patrick Mangi wa Shirika la Masista wa Mtakatifu Theresa wa Mtoto
Yesu, Jimbo Katoliki Iringa, ambaye kitaaluma ni daktari wa binadamu, katika Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani, anawaalika Watawa, lakini Wanovisi na Walelewa kwa namna ya pekee
kuhakikisha kwamba, wanakuwa na imani, matumaini na mapendo thabiti kwa Mungu na watu
wote ambao Mama Kanisa atawakabidhi ili kuwahudumia.
Wanapaswa
kuwa na ujasiri katika kumtangaza Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka
katika wafu, kiini na chemchemi ya imani ya Kanisa. Katika maisha yao, watu wamwone
Kristo aliye hai katika nafsi zao.
Anawashukuru na kuendelea kuwaombea wazazi
wa watawa, wanovisi na walelewa. Anawahimiza wazazi kutambua na kutekeleza wajibu
na dhamana waliyokabidhiwa na Mama Kanisa ya kuhakikisha kwamba, Familia inakuwa ni
Kanisa dogo la nyumbani, kitalu cha miito, shule ya utakatifu, haki, amani, upendo
na msamaha.
Wazazi wajikite katika kurithisha imani na tunu msingi za maisha
ya Kikristo na kiutu zitakazomwilishwa na watawa wakati wa kutekeleza maisha na utume
wao ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla.