2013-07-15 08:17:20

"Bara la Afrika linawaka moto!"


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM katika mkutano wake wa kumi na sita, uliokuwa unafanyika mjini Kinshasa, DRC, imekuwa ni fursa kwa wajumbe wa SECAM kupembea kwa kina na mapana, Kanisa kama Familia ya Mungu inayokiri na kuungama: Ubatizo na imani moja katika Fumbo la Utatu Mtakatifu na Neno la Mungu, inavyowajibika katika kutunza na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho Barani Afrika. RealAudioMP3

Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican mjini Kinshasa, DRC anasema kwamba, Bara la Afrika kwa sasa linawaka moto kutokana na kinzani za vita, migogoro ya kijamii, kitamaduni, kisiasa na kidini; kuna ukosefu mkubwa wa haki msingi za binadamu; rasilimali na utajiri wa Bara la Afrika unaendelea kupokwa na wajanja wachache; rushwa na ufisadi ni mambo ambayo kwa sasa yamekuwa ni wimbo usiokuwa na mchezaji!

Kanisa Barani Afrika limebainisha mbinu mkakati utakaoliwezesha kuwa kweli ni chombo cha haki, amani na upatanisho, kama sehemu ya utekelezaji wa mikakati ya kichungaji iliyobainishwa na Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika na hatimaye, hati baada ya Sinodi hii ikatolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Haki, amani na upatanisho ni tunu muhimu sana katika maisha ya mwanadamu katika ngazi mbali mbali.

Askofu Ngalalekumtwa anasema, kila mtu anachangamotishwa na Mama Kanisa kuwa ni chombo cha haki, amani na upatanisho Barani Afrika. Amani inapaswa kupata chimbuko lake katika undani wa moyo wa mwanadamu. SECAM imepitisha maazimio katika utekelezaji wa Waraka wa Dhamana ya Afrika, Africae Munus iliyotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Waraka huu si mapambano ya meza wala makabati, bali unapaswa kutekelezwa ili dunia iwe na amani na Bara la Afrika liweze kutoa mchango wake katika kurejesha misingi ya haki, amani na upatanisho.







All the contents on this site are copyrighted ©.