2013-07-13 07:50:31

Cheche za Mwanga wa matumaini kutoka kwa Mwenyeheri Yohane Paulo II


Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani ni cheche ya mwanga wa matumaini na zawadi kubwa ambayo Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili ameliachia Kanisa na kwamba, matunda ya Maadhimisho haya ni juhudi za mikakati ya shughuli za kichungaji zinazotekelezwa na Mabaraza ya Maaskofu katoliki sehemu mbali mbali za dunia, kabla, wakati na baada ya Maadhimisho haya! RealAudioMP3

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 yana umuhimu wa pekee kwani, kunako mwaka 1987, kwa mara ya kwanza Siku ya Vijana Duniani iliadhimishwa huko Buenos Aires, nchini Argentina. Hapa watu wakashuhudia vijana wakiungana na Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili, aliyewaambia vijana kwamba, yuko kati yao, ili kuwasikiliza, kuzungumza na kusali pamoja nao! Vijana ni jeuri na matumaini ya Kanisa, changamoto kwa vijana kuwa ni waaminifu kwa Kristo na Kanisa lake. Vijana wanahamasishwa kuwa makini dhidi ya wote wanaotaka kufisha matumaini yanayobubujika kutoka katika undani wa mioyo yao!

Hii ni tafakari ya kina inayotolewa na Kardinali Stanislaw Rylko, Rais wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Walei. Anasema, Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani yaliandaliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita na sasa itaadhimishwa na Papa Francisko, Myesuiti wa kwanza kuchanguliwa kuwa ni Khalifa wa Mtakatifu Petro na na Papa wa kwanza kutoka Amerika ya Kusini.

Baba Mtakatifu Francisko anawaambia vijana kwamba, anaungana na watangulizi wake, Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika Maadhimisho haya, kwa imani na matumaini makubwa. Ili kufanikisha Maadhimisho haya, Baba Mtakatifu Francisko alikuwa amewaalika vijana kujiandaa kikamilifu kiroho, kwa kutambua kuwa hili ni tukio la kiimani na hija ya maisha ya kiroho. Ni mwaliko kwa vijana kutoka katika undani na utupu wa maisha yao ya vijana ili kuwaendele wengine wanaoishi na kusukumizwa pembezoni mwa Jamii kwani njia za Bwana zina maajabu mengi.

Maadhimisho ya Mwaka 2013 huko Rio de Janeiro, Brazil yanaongozwa na kauli mbiu ”Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi”. Huu ni mwaliko anasema Kardinali Rylko kwa vijana kukuza na kudumisha moyo wa kimissionari ndani mwao, huku wakiendelea kuchangamotishwa na ujumbe wa Mababa wa Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Uinjilishaji Mpya kwamba, mchakato wa Uinjilishaji mpya unapania kutangaza Imani ya Kikristo.

Vijana wanaotoka Amerika ya Kusini wanahamasishwa pia kuwani Wamissionari katika nchi zao, kwani vijana wana kiu ya kutaka kusikiliza Habari Njema ya Wokovu ikitangazwa miongoni mwao kwa njia ya ushuhuda wa maisha na imani tendaji. Vijana wanapaswa kutambua kwamba, utume na maisha ya Kanisa yako mikononi mwa vijana wenyewe! Ni dhamana ya Mama Kanisa kuhakikisha kuwa inaibua mbinu mkakati utakaofanikisha kuasha dhamiri nyofu, ari na moyo wa kimissionari; miito na huduma ndani ya Kanisa mintarafu mwongozo na Mafundisho Jamii ya Kanisa.

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 yanakwenda sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, mwaliko na changamoto kwa vijana kutambua mafundisho tanzu ya Kanisa; kukiri imani kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya uhsuuda wa maisha adili; Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa na Sala. Vijana wajitaabishe kuifahamu Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki; muhtasari wa: Imani, Sakramenti za Kanisa, Amri za Mungu na Maisha ya Sala.

Hii ni amana ya Kanisa iliyohifadhiwa kwa zaidi ya miaka elfu mbili iliyopita. Vijana wanaalika kujisomea na kutafakari Katekesimu Mpya ya Kanisa Katoliki kwa moyo mkuu na endelevu. Kanisa Katoliki nchini Brazil linawasubiri vijana kwa moyo wa upendo na ukarimu

Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani si haba! Kanisa linaweza kufanya tathmini ya kina ili kuangalia ni matunda yepi ambayo yamekwishajitokeza katika kipindi chote hizi na wapi ambapo Kanisa linapaswa kuboresha ili kufanikisha Maadhimisho haya. Vijana wanapaswa kugundua kwamba, Yesu ni njia, ukweli na uzima; Kanisa kwa upande wake ni Mama, Mwalimu na Rafiki wa kweli. Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kiongozi ni mwenza wa hija ya maisha ya kiroho na kiutu; ni rafiki ambaye vijana wanaweza kumtumainia. Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani ni maabara au karakana za imani, kama alivyopenda kusema, Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, enzi zake!

Hapa pamekuwa ni chemchemi na chimbuko la miito mbali mbali ndani ya Kanisa na kwamba, Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, limejikuta likiwa na sura ya ujana, pasi na makunyanzi; Kanisa ambalo limewasukuma vijana kuendelea kujiamisha kwa Kristo na Kanisa lake. Vijana kwa nyakati hizi wamekuwa kweli wadau wa heri za Mlimani, Manabii wa nyakati hizi na vyombo vya upendo wa Mungu kwa binadamu.

Vijana watambue kwamba, Maadhimisho ya Siku za Vijana Duniani ni zawadi ya Mungu kwa Kanisa lake; mahali ambapo vijana wanaweza kuchota tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kitamaduni; ni chombo muhimu sana cha Unjilishaji Mpya; mahali ambapo wenye kiu na njaa ya maisha ya uzima wa milele wanaweza kushibishwa!

Hili ni Jukwaa la majadiliano kati ya Kanisa na Vijana, changamoto kwa pande hizi mbili anasema Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili, kusikilizana kwa makini. Hiin i epifania na ufunuo wa imani; ni mahali pa kupanga na kutekeleza mikakati ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya vijana. Hii ni amana na urithi mkubwa kutoka kwa Papa Yohane Paulo wa Pili kwa ajili ya Kanisa.

Maadhimisho ya Mwaka huu anasema Kardinali Stanislaw Rylko ni njia ya kuona dhamana ya Uinjilishaji Mpya na fahari ya kuwa Mkristo. Wachunguzi wa mambo wanaendelea kusema kwamba, Rio mwaka huu hapatoshi, kwani wanategemea kwamba, Baba Mtakatifu Francisko, atafunika! Kwani ameonesha upendo na matumaini makubwa kwa vijana. Anawakumbusha kwamba, wao ndiyo furaha na chemchemi ya imani, kwa njia ya uwepo wao Kanisa kamwe haliwezi kuzeeka. Ni changamoto ya kutumia karama na vipaji walivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Kanisa na Jamii inayowazunguka.

Vijana kamwe, wasiogope kuwa na ndoto kubwa na wasikubali baadhi ya watu kuwapokonya matumaini yanayobubujika kutoka katika undani wa maisha yao! Wawe na ujasiri wa kukumbatia zawadi ya maisha. Kwa maneno machache Papa Francisko ameonesha umahiri mkubwa wa kuzungumza na vijana, kwa kweli watu wanasubiri makali yake!

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani nchini Brazil yanawahamasisha vijana kuwa na ari na moyo wa kimissionari. Wasikilize kwa umakini mkubwa Katekesi na Mafundisho yatakayotolewa ili hatimaye, waweze pia kuwashirikisha vijana wenzao. Neno la Mungu liwe ni dira na taa inayoangaza mapito yao! Wasisahau kujipatanisha na Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho, ili kuonja huruma na upendo wa Mungu. Fumbo la Msalaba liwakumbushe vijana: mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, kiini cha imani ya Kanisa.

Vijana wanapaswa kuonjeshwa ushuhuda wa imani tendaji ili waweze kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Kristo na Kanisa lake. Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani ni dawa inayoponya mchoko wa watu kuendelea kuamini kwa kuamsha ari na moyo mpya wa Kimissionari, ambao unawawezesha vijana kuwa ni vyombo madhubuti vya Uinjilishaji.

Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.