2013-07-13 11:50:51

Amani ni jina jipya la maendeleo endelevu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania litaendelea kuwekeza katika sekta ya elimu, ili kuhakikisha kwamba, watanzania wanapata elimu bora, itakayowasaidia kupambana na changamoto za maisha kwa ari na ujasiri mkubwa.

Hayo yamebainishwamwishoni mwa juma katika hafla ya kuchangia Kituo cha Mwalimu Julius Nyerere, kilichoko kwenye Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afya na Sayansi Mwambata, Bugando, Mwanza. Kituo hiki kitakapokamilika, kitakuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 800. Ujenzi wa awamu ya kwanza unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi billioni 3/. Hiki kitakuwa ni kituo cha tafiti kinachotarajiwa kuhudumia wadau mbali mbali katika sekta ya tiba na dawa nchini Tanzania.

Rais mstaafu Benjamin William Mkapa wa Tanzania ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika uwekaji wa jiwe la msingi la Kituo cha Mwalimu Julius Nyerere, CUHAS. Amewataka watanzania kuendelea kusali kwa ajili ya kuombea misingi ya haki, amani na utulivu nchini Tanzania. Hizi ni tunu msingi zilizohubiriwa na kumwilishwa na Mwalim Nyerere katika maisha na uongozi wake kama Rais wa Tanzania.

Naye Mheshimiwa Padre Charles Kitima, aliyekuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha SAUT amesema, bila: haki, amani na utulivu, hakuna maendeleo na kwamba, afya ya wananchi itasuasua tu: Kumbe, amani na utulivu ni jina jipya la maendeleo ya mwanadamu kiroho na kimwili.







All the contents on this site are copyrighted ©.