Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 15 ya Kipindi cha Mwaka C. wa Kanisa
Ninakuleteeni Tafakari ya Neno la Mungu Dominika ya 15 ya Kipindi cha mwaka C wa Kanisa.
Leo Mama Kanisa ametuwekea Neno la Bwana akitufudisha Amri kuu ya Mapendo yaani kumpenda
Mungu na kumpenda jirani. Mwinjili Luka anasema, Mungu ni mkuu mno kumbe kumpenda
yeye lazima kujidhihirishe pia katika kumpenda jirani yetu.
Katika Injili
ya Dominika hii jirani ni awaye yote mwenye taabu na masumbufu mbalimbali katika maisha.
Ni yule anayehitaji msaada wako, asiye na chakula, asiye na mahali mahali pazuri pa
kuishi. Bwana anatoa fundisho hili baada ya kuulizwa swali na mwanasheria juu ya namna
gani aweza kuurithi uzima wa milele. Bwana akitambua hila yake anajibu swali hilo
kwa kuweka swali mbele ya mwansheria na swali hilo linalala katika kile anachokifahamu
mwanasheria huyu. Bwana anasema Torati yatufundisha nini juu ya hilo? Mwanasheria
atajibu akisema mpende Bwana Mungu wako na jirani yako.
Baada ya jibu la mwanasheria
Bwana akitambua yakuwa lazima fundisho lake likae katika mazingira halisia ili liweze
kueleweka vema, anafundisha akitumia mfano wa Msamaria mwema. Basi Bwana anatoa mfano
huo akianza na mtu mmoja ambaye hatumjui jina lake anayetelemka toka Yerusalemu kwenda
Yeriko. Mtu huyu anavamiwa na wanyang’anyi na kuumizwa vyakutosha na anaachwa barabarani
ambapo baadaye watapita watu wa aina mbalimbali walio katika makundi matatu. Mtu huyu
kwa hakika huwakilisha wale wote walio katika taabu na mateso mbalimbali ya kiroho
na kimwili katika maisha yao. Kisha kumweka mtu huyu katika mtililiko wa mafundisho
yake ataweka sasa makundi ya watu wanaopita mahali ambapo mtu huyo alikuwa amesukumizwa
kandokando ya barabara.
Mpendwa msikilizaji, kundi la kwanza na la pili yaani
Kuhani na Mlawi yanaonesha hisia ileile na kundi la tatu yaani la Msamaria linaonesha
hisia tofauti. Kundi la kwanza na la pili wanapita pale alipo mwenye taabu na hawaoneshi
fikra yoyote yakutaka kumsaidia ndugu huyu mwenye taabu. Makundi haya mawili si kwamba
hawana upendo bali wanafikiria na kuuona upendo kama jambo ambalo lazima likae katika
mpango unaoendana na uchaguzi, maana yake wanachagua nani anasitahili huduma yao,
kulingana na muda mwafaka na hata ikiwezekana kimahesabu.
Mpendwa, jambo hili
ni la ajabu, upendo wawezaje kuwekwa katika vipimo vya kimahesabu na muda? Kwa hakika
haiwezekani kuwa na jambo la namna hiyo. Kwa maana jirani si yule ambaye mara zote
unamfahamu bali yule unayekutana naye pasipo kutarajia, ni yule anayepangua mipango
yako ya maendeleo, ni yule anayejeruhi ratiba yako uliyoipanga! Kwa namna hiyo usemi
huu waweza kuwa wa kweli “utampenda Bwana kwa uwepo wako wote na utampenda yule usiyemtarajia
kama unavyojipenda mwenyewe”
Mpendwa msikilizaji, kundi la tatu ni lile la
Msamaria mwema. Wote twatambua uhusiano kati ya Wayahudi na Wasamaria. Wasamaria mbele
ya Wayahudi ni watu wasio na elimu, ni watu wa kutengwa na ni wazushi, kumbe ilikuwa
lazima kuwaepuka. Ni katika mantiki hiyo basi Msamaria angekuwa wa kwanza kumkwepa
huyu mteswa wa njiani!
Badala yake anasimama na kutoa huduma baada ya kuguswa
moyoni mwake na taabu ya mwingine. Yeye haweki upendo katika mahesabu wala haangalii
muda gani atapoteza anachotazama ni wokovu wa mtu huyu. Upendo huvumlia, upendo huaanza
moyoni na humalizikia katika kutoa huduma. Msamaria huyu haishii katika kutenda peke
yake bali anamshirikisha mwingine taabu hiyo,yaani mwenye hotel. Mpendwa mwana wa
MUngu mwenye hotel anawakilisha mfumo wa kijamii ambao kama haupo huruma na upendo
wetu hubaki katika ubinafsi pasipo kufikia lengo lake! Ni kwa namna hiyo basi mifumo
jamii inahitaji kushtuliwa ili ukamilifu wa maisha ya mapendo uweze kufikia kilele
chake.
Mpendwa msikilizaji wajifunza nini toka fundisho hili la Bwana? Wapi
unatakiwa kufika baada ya kutafakari mfano huu? Kwa hakika lengo ni kutaka kukufikisha
katika upeo wa kupambanua kuwa Msamaria mwema namba moja ni Yesu mwenyewe, ndiye amekuwa
karibu na wateswa na maskini na wafungwa, akitaka kuwaondoa na amewaondoa kweli katika
taabu zao. Lk 4:18. Basi nasi tukiwa wana wa Mungu twaitwa kujifungamanisha katika
Bwana tukiyachuchumalia mafundisho hayo ya Bwana. Nikutakie yote mema katika kujitahidi
kuwa Msamaria mwema.
Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako
na Pd. Richard Tiganya C.PP.S.