2013-07-12 09:20:44

SIDA kugharimia Mpango wa Maendeleo 2013 - 2019


Tanzania itafaidika na mpango wa maendeleo wa miaka mitano unaogharamiwa na Serikali ya Sweden utakao gharimu kiasi cha T.Shs trilioni 1.4 kupitia kitengo chake cha Swedish International Cooperation Agency (SIDA). Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Mheshimiwa Lennarth Hjelmaker amemueleza Rais Jakaya Kikwete Ikulu ambapo alifika kumkabidhi Rais barua kutoka kwa Waziri wa Maendeleo ya Kimataifa wa Sweden Mheshimiwa Gunilla Carlsson, ambaye amemwandikia Rais Kikwete barua maalum kumjulisha kuhusu mpango huo ambao Serikali ya Sweden utaugharamia.

Mpango huo wa maendeleo wa 2013-2019 unalenga katika maeneo makuu matatu:
·Kuongeza ajira, kuendeleza sekta ya nishati na masoko kwa mazao ya kilimo;
·Elimu ambapo kipaumbele kitakuwa katika kuwapa elimu ya awali watot wengi zaidi na pia katika vyuo vya ufundi;
·Kukuza demokrasia, uwajibikaji na uwazi pamoja na kuongeza uelewa wa haki za binadamu nchini.

Katika barua yake kwa Rais Kikwete, Waziri Carlsson amemueleza Rais Kikwete kuwa Tanzania itaendelea kuwa mwenza muhimu kwa nchi ya Sweden “Huu si ushahidi wa ushirika wetu wa kihistoria, bali pia ni kwa ajili ya sera za Tanzania na ukuaji wa taasisi za kidemokrasia nchini Tanzania” amesema Waziri Carlsson na kuongeza kuwa “Wakati uhusiano baina ya nchi hizi mbili ni muhimu, mahusiano yetu ya baadaye yataimarika zaidi sio kwenye misaada bali katika uwekezaji” ameongeza.

Rais Kikwete ameishukuru Sweden kwa msaada huo na kueleza kuwa nchi zinazoendelea kwa hakika zinahitaji misaada ya maendeleo ili kujijengea uwezo na hatimaye, kufikia kwenye uwekezaji ambao utaharakisha maendeleo ya nchi hizi.








All the contents on this site are copyrighted ©.