2013-07-12 11:29:34

Padre ni Mwalimu wa mambo ya Kimungu, Kuhani anayeadhimisha Mafumbo ya Kanisa na Mchungaji mwenye moyo wa upendo na huruma!


Katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Benedikto Abate, hapo tarehe 11 Julai 2013 ambaye katika Kanuni za maisha ya kitawa alikazia sala na kazi, Jimbo Katoliki la Dodoma, limemwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa Maadhimisho ya Miaka 17 tangu Askofu Gervas Nyaisonga alipopewa Daraja Takatifu la Upadre. Waamini wanamwombea ili aendelee kuwafundisha, kuwatakatifuza na kuwaongoza kadiri ya moyo na mapenzi ya Kristo, Mchungaji mkuu. RealAudioMP3

Askofu mstaafu Mathias Isuja wa Jimbo Katoliki la Dodoma, alitoa Sakramenti ya Daraja takatifu la Upadre kwa Shemasi Laurent Lelo baada ya kuhitimu masomo na majiundo yake ya Kipadre: Seminari kuu ya Ntungamo iliyoko Jimbo Katoliki la Bukoba na Kipalapala iliyoko Jimbo kuu la Tabora. Itakumbukwa kwamba, alipewa Daraja la ushemasi hapo tarehe 13 Januari 2013 na Askofu mstaafu Mathias Joseph Isuja.

Askofu mstaafu Isuja anasema, Shemasi Laurent Lelo anapewa Daraja Takatifu la Upadre, wakati huu wa ukame wa miito ya Kipadre, sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani unaoendelea kuibua changamoto mbali mbali katika maisha na utume wa Kanisa. Ni mwaliko wa kuendelea kusikiliza sauti ya Kristo anayesema kwamba, mavuno ni mengi, lakini watenda kazi katika shamba la Bwana ni wachache, basi waendelee kumwomba Bwana wa mavuno ili apeleke watenda kazi, wema, watakatifu na wachapakazi katika shamba lake.

Askofu mstaafu Isuja, amemkumbusha Shemasi Lelo kwamba, ameitwa, akatakaswa na kutumwa na Mwenyezi Mungu kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Yeye anashiriki Nafsi ya Kristo kwa kuwa: kuhani, mwalimu na mchungaji. Anapaswa kuwa ni Kuhani kwa mfano wa Melkisedeki aliyekuwa mchamungu na mtu wa amani. Kama Padre anatumwa kuwa mwalimu wa mambo ya Kimungu na wala si "kufundisha sera zake", ndiyo maana anapaswa kulifahamu, kuliishi na kulitangaza Neno la Mungu.

Kama Padre anatumwa kuwatakasa watu kwa njia ya Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa, kamwe watu wasitindikiwe na neema na baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kwa vile tu, Padre amemezwa na malimwengu hana muda wa kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa.

Kama Mchungaji kwa moyo na ari ya Kristo anapaswa kujivika huruma na upendo kwa kuzikabili changamoto za ulimwengu kwa njia ya: Sala, Tafakari ya Neno la Mungu na Maisha adili. Aendelee kumtegemea Roho Mtakatifu atakayemkirimia matunda ya Roho Mtakatifu kama yalivyobainaishwa kwenye Maandiko Matakatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.