2013-07-11 14:21:31

Mabadiliko ya Sheria za makosa ya jinai na kazi yatolewa mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko kwa utashi wake mwenyewe, tarehe 11 Julai 2013 amefanya mabadiliko katika baadhi ya sheria za makosa ya jinai na adhabu katika makosa ya kiutendaji ambazo zimekuwa zikitumika mjini Vatican. Sheria ambazo zilikuwa zikitumika kwa ajili ya Tume ya Kipapa ya Mji wa Vatican, sasa zitaanza kutumika katika shughuli zote zinazotekelezwa na Vatican.

Sheria hizi mpya ni mwendelezo wa mageuzi ya sheria za Vatican yaliyoanzishwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kunako mwaka 2010. Hizi ni sheria ambazo kwa sasa zinakidhi viwango vya kimataifa pamoja na kuzingatia itifaki ya Mwaka 1949 kuhusu vita na makosa ya kivita. Itifaki ya mwaka 1965 kuhusu ufutwaji wa aina zote za ubaguzi wa rangi; itifaki ya mwaka 1984 inakataza mateso na ukatili dhidi ya binadamu na adhabu kali; Itifaki ya mwaka 1989 inabainisha kuhusu haki za mtoto pamoja na itifaki ya mwaka 2000.

Sheria hizi zinafafanua kwa kina kuhusu makosa dhidi ya ubinadamu, kwa kujikita zaidi katika: mauaji ya kimbari mintarafu ufafanuzi uliotolewa na Mahakama ya Kimataifa. Kumefanyika pia marekebisho ya sheria dhidi ya makosa yanayotendwa na mtu anapokuwa kazini mintarafu mikakati ya Umoja wa Mataifa kupambana na rushwa. Adhabu ya kifungo cha maisha imefutwa na badala yake adhabu ya juu itakuwa ni kati ya miaka 30 hadi 35 jela.

Sheria mpya zinawabana wafanyakazi wa mahakama wanaoweza kujinufaisha kwa nafasi na madaraka waliyonayo katika vituo vyao vya kazi. Katika mfumo mzima wa sheria, jambo la kwanza katika mchakato huu ni mhusika atahesabiwa kuwa ni mtuhumiwa hadi pale itakapobainika kwamba, ametenda kosa. Mahakama imepewa madaraka ya kuweza kutaifisha mali ya watuhumiwa. Sheria zinazohusu ushirikiano wa kimataifa zimeboreshwa kwa kuzingatia itifaki za kimataifa zilizotolewa hivi karibuni.

Sheria na adhabu kuhusu utekelezaji wa majukumu zina asili ya jumla, ili kutoa mwelekeo wa jumla kuhusu adhabu zinazoweza kutolewa katika maeneo mbali mbali, kama njia ya kuhakikisha kwamba, sheria na mafao ya Jamii yanalindwa. Kimsingi, sheria hizi zinapania pamoja na mambo mengine kuboresha mfumo wa sheria za Vatican kwa kusoma alama za nyakati pamoja na kuongeza tija na ufanisi.







All the contents on this site are copyrighted ©.