"Nimeguswa na Ibada ya Misa Takatifu na Baraka kutoka kwa Papa Francisko, zawadi kubwa
katika hija ya maisha yangu ya imani"
Francis Kilenga, Afisa Miradi wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, Vikarieti
ya Tanzania, yenye makao yake makuu mjini Dodoma katika mahojiano na Radio Vatican
anakiri kwamba, kati ya matukio makubwa yaliyogusa hija ya maisha yake ni kushiriki
Ibada ya Misa Takatifu pamoja na kupata baraka za Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili
tarehe 7 Julai 2013.
Francis Kilenga
anasema kwamba, hili ni tukio ambalo kwa hakika atalikumbuka katika hija ya maisha
yake ya kiroho na kwamba, limeacha chapa ya kudumu katika maisha yake kama Mkristo,
hasa wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani.
Mzee Kilenga alikuwa
nchini Ujerumani na Italia kama sehemu ya shughuli zake kwa ajili ya kujadiliana na
Mashirika mbali mbali ya Misaada ya Kanisa Katoliki kwa ajili ya kuongezea nguvu katika
mchakato wa utoaji wa huduma makini, wakati huu Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi
ya Yesu, linapojielekeza kusikiliza kilio cha damu, kutoka kwa maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii.