2013-07-10 08:27:46

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kiwe ni kichocheo cha Vijana wa Kikristo kuwa wafuasi wa Kristo na Wamissionari mahiri!


Nia ya jumla ya Baba Mtakatifu kwa Mwezi Julai inajikita zaidi katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa mwaka 2013 itakayoadhimishwa nchini Brazil, ili iwe ni kichocheo kwa vijana wa Kikristo kuwa ni wafuasi wa Kristo na Wamissionari wa Injili. RealAudioMP3

Baba Mtakatifu katika nia yake ya Kimissionari anaielekeza zaidi Barani Asia, ili liweze kufungua malango yake kwa wajumbe wa Injili. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika Waraka wake kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Mlango wa Imani, “Porta Fidei” anawaalika waamini kwa namna ya pekee, kuwa ni mng’ao wa Neno la Ukweli.

Hii ndiyo hija ya maisha iliyooneshwa na Kristo alipokutana na yule mwanamke Msamaria pale kisimani, akamwomba maji ya uzima wa milele. Katika mahojiano na Yesu, yule mwanamke akamfungulia Yesu hazina ya moyo wake naye Kristo akazima ile njaa na kiu iliyokuwa imejikita katika moyo wa yule mwanamke, kiasi kwamba, akapata ari na mwamko wa kwenda kuwashirikisha wengine ile furaha ya Habari Njema ya Wokovu inayobubujika kwa kukutana na Yesu Kristo!

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, anasema, hii ndiyo changamoto iliyoko mbele ya Wakristo kwa sasa, kwani wanahamasishwa kushiriki katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaozamisha mizizi katika maisha na utume wa Kanisa. Waamini watambue kwamba, wao ndio walengwa wakuu wa Injili na pia wanatumwa Kuwainjilisha wengine! Kiini cha Injili ni Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu na kwamba, Yeye ndiye Mkombozi wa dunia.

Yesu ni Neno wa Mungu aliyetumwa ulimwenguni, akajitoa bila ya kujibakiza kwa njia ya Fumbo la Umwilisho, kwa kujitwalia hali ya unyonge wa mwanadamu, akaupenda na kuukomboa kutoka katika dhambi na mauti kwa njia ya Fumbo la Msalaba! Imani kwa Mwenyezi Mungu ni kazi ya upendo iliyotekelezwa na Yesu na kwamba, hii ni zawadi na fumbo ambalo linapaswa kukaribishwa moyoni na katika uhalisia wa maisha, kama alama ya shukrani kwa Kristo.

Imani ni zawadi ambayo mwamini anaalikwa kuishirikisha kwa wengine; ni karama inayopaswa kuendelezwa ili iweze kuzaa matunda; ni mwanga unaopaswa kung’ara katika maisha ya watu! Hii ni zawadi muhimu sana katika historia na maisha ya mwanadamu mintarafu uwepo wa Kristo anayeponya, safisha na kudhihirisha uwepo wake unaotuliza shida na mahangaiko ya maisha ya mwanadamu.

Kutokana na changamoto zote hizi, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, anasema, waamini wanapaswa kuwa makini zaidi na hali halisi kwa wakati huu, ili kuibua mbinu mkakati wa kichungaji utakaoliwezesha Kanisa kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa moyo na ari kubwa zaidi kwa kuendelea kusoma alama za nyakati. Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, kila mwamini na Jumuiya ya Waamini inajikita katika Injili ya Kristo, hasa nyakati hizi ambako kuna mabadiliko makubwa yanayoendelea kutokea sehemu mbali mbali za dunia.

Kati ya changamoto kubwa zinazoukabili mchakato wa Uinjilishaji Mpya ni ukanimungu na watu kumezwa mno na malimwengu. Lakini, hata katika mazingira na hali kama hii, anasema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, cha ajabu ni kuona kwamba, kuna watu wenye kiu na njaa ya uwepo wa Mungu, wanaosubiri kumegewa Mkate wa Uzima wa Milele na Kupewa Maji yanayozima kiu ya maisha na utupu wa mwanadamu, kama ilivyokuwa kwa yule mwanamke Msamaria.

Kwa ufupi hizi ndizo nia za jumla na za kimissionari za Baba Mtakatifu kwa Mwezi Julai.








All the contents on this site are copyrighted ©.