2013-07-09 09:11:06

Vijana msipende kuzamia, mtakumbunana na kifo!


Queen Said ni mratibu wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio nchini Tanzania. Katika mahojiano maalum na Radio Vatican kuhusu tatizo la vijana kutoka nchi zilizoendelea na kwa namna ya pekee kutoka Barani Afrika kupenda kuzamia Ulaya na Marekani wakitafuta malisho ya kijani kibichi anasema, kila mtu anayo haki ya kubaki na kuishi katika nchi yake mwenyewe. Kwa njia hii vijana wanaweza kutumia fursa na rasilimali iliyopo nchini mwao kujiendeleza wenyewe, kwa ajili ya familia na nchi zao katika ujumla wake. RealAudioMP3

Queen Said ambaye bodo ni kijana kabisa aliyehitimu masomo yake hivi karibuni na kwa sasa anafanya kazi kwenye Hospitali ya Rufaa ya KCMC, Moshi, Mkoani Kilimanjaro, Tanzania anapenda kuwashauri vijana wenzake wenye mawazo ya kuzamia ughaibuni wakidhani kwamba, wataweza kupata maisha bora zaidi, kuachana na ndoto kama hizi, kwani wengi wao wanapofika Ulaya na Marekani wanakumbana na adha, madhulumu, nyanyaso na kwa sehemu kubwa kifo, kama inavyojitokeza sehemu mbali mbali za dunia.

Vijana hao mara nyingi wanajikuta wakiangukia kwenye mikono ya wafanyabiashara haramu ya binadamu. Wakiwa nchini mwao, wana uwezo na fursa nyingi za kuweza kukabiliana na changamoto za maisha, kumbe, ushauri mkuu ni kwa vijana kubaki nchini mwao ili waweze kujiendeleza. Maisha Ulaya na Marekani ni tofauti kabisa na vile yanavyooneshwa kwenye Luninga na vyombo mbali mbali vya mawasiliano ya Jamii. Anasema, "usiwaone Wamasai wamevaa lubega rangi nyekundu ukadhani wote ni washabiki wa Timu ya Simba"! Huo ni utamaduni na mavazi yao!

Queen Said anasema, kuna sababu nyingi zinazopelekea watu kuzikimbia nchi zao: maafa asilia, vita, kinzani, hali mbaya ya uchumi, madhulumu na nyanyaso mbali mbali, yote haya ni mambo yanayopaswa kuangaliwa kwa jicho la mshikamano unaoongozwa na kanuni ya auni.

Serikali za nchi mbali mbali zitambua na kuthamini utu na heshima ya kila mkimbizi anayeomba hifadhi ya maisha yake, kwa kuzingatia sheria, kanuni na mikataba ya kimataifa. Ikumbukwe kwamba, hata wakimbizi katika shida na mahangaiko yao, wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, wana utu na heshima yao kama binadamu!







All the contents on this site are copyrighted ©.