2013-07-08 07:46:12

Vijana jengeni ari na moyo wa kimissionari


Katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, Kanisa linapaswa kujikita zaidi na zaidi katika maisha ya utume wa kimissionari, tayari kwenda sehemu mbali mbali za dunia kutangaza Habari Njema ya Wokovu, daima likiendelea kutembea katika njia ya uaminifu mintarafu maagizo ya Kristo mwenyewe. Ni changamoto na mwaliko kwa vijana kushiriki kikamilifu katika maisha ya kitawa na kimissionari.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko kwa umati mkubwa wa Majandokasisi, wanovisi na vijana ambao wako kwenye majiundo ya maisha na utume wa Kipadre na Kitawa, waliokuwa wamekusanyika mjini Vatican kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Tafakari ya Baba Mtakatifu ili sheheni majadiliano ya kina kati ya vijana, kwa kuwataka kuwa makini na malimwengu yanayoweza kuwapotosha katika safari ya maisha yao ya kiroho na kiutu.

Wajipange barabara na kamwe wasifanye mambo kwa kubahatisha kwani hali kama hii ina hatari kubwa katika maisha na ustawi wa vijana. Vijana wajipange na hatimaye, wachague wito wanaotaka kufuata katika maisha yao, ikiwa ni maisha ya ndoa na familia, basi wahakikishe kwamba, wanakuwa ni wazazi bora na mafano wa kuigwa na jirani zao. Ikiwa kama watachagua kuwa ni Mapadre na Watawa, basi wajitose kimaso maso bila ya kujiachilia kwa ajili ya Mungu na jirani.

Vijana wajisikie kuwa na furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe na wala si kwa vile wanamiliki simu nzuri ya kiganjani, Pikipiki ambayo ikipita mtaani kila mtu "anakata shingo" au kwa kuwa na gari la kifahari. Yote haya ni mambo ya mpito anasema Baba Mtakatifu Francisko na kamwe hayawezi kumpatia kijana furaha ya kweli katika maisha!

Anasema, anasikitishwa kuona jinsi ambavyo Mapadre na Watawa wanavyokimbilia kuwa na magari ya fahari. Anatambua umuhimu wa gari kwa ajili ys shughuli za kichungaji, lakini kuna haja ya kuwa na busara na kiasi katika manunuzi na matumizi ya vyombo vya usafiri, kwa kutambua kwamba, kuna watu wanaoteseka sehemu mbali mbali za dunia, watu ambao wanahitaji kuonja: upendo, huruma na ukarimu kutoka ndani ya Kanisa.

Baba Mtakatifu anawakumbusha vijana kwamba, wao ni muhimu na watu wa maana sana mbele ya Mwenyezi Mungu, ndiyo maana amewachagua ili waweze kushiriki katika utume wa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, kama Mapadre, watawa na Wamissionari. Wao wanapaswa kutoa jibu makini, linaoonesha upendo wao kwa Mwenyezi Mungu.

Hii ndiyo siri ya furaha ya vijana wanaojitosa kimaso maso kwa ajili ya Mungu na jirani. Ni mwaliko wa kuchuchumilia utakatifu wa maisha kwa kuishi kwa uaminifu mashauri ya Kiinjili; yaani: Utii, Ufukara na Useja, mambo yanayoonesha ubaba na umama katika utekelezaji wa mikakati ya shughuli za kichungaji. Waseminari na Watawa watambue kwamba, upendo wao kwa Yesu ni wa hali ya juu kabisa kwani unamwilishwa katika Mashauri ya Kiinjili na kamwe wasiwe ni Mapadre na Watawa wasiokuwa na furaha kana kwamba, wameonjeshwa pili pili kichaa! Uzuri wa maisha ya Kipadre na Kitawa ni ile furaha ya kweli inayojikita katika uaminifu kwa Mungu, Kanisa na Jirani, kama kielelezo makini cha ushuhuda wa Injili.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika Waseminari na Wanovisi kushiriki kikamilifu katika Sakramenti za Kanisa na kwa namna ya pekee Sakramenti ya Upatanisho, inayowaonjesha upendo na huruma ya Mungu isiyokuwa na kifani. Wasiogope kukiri dhambi zao, ili kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao. Hapa kuna haja ya kukazia fadhila ya ukweli na uwazi.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, katika majiundo ya Kipadre na Kitawa kuna mambo makuu manne yanayopaswa kuzingatiwa yaani: majiundo na maisha ya kiroho; majiundo ya kiakili na maisha ya kitume; mambo yatakayowawezesha vijana hao kutekeleza dhamana na wajibu wao wa kutangaza Injili kwa ari na moyo mkuu kabisa, daima wakitambua kwamba, wanapaswa kuishi katika Jumuiya. Hizi ni nguzo msingi katika ujenzi wa maisha ya kipadre na kitawa. Baba Mtakatifu amewaonya Waseminari na Wanovisi kutojiingiza katika mambo ya umbea kwani wambea hawana bunge!

Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake kwa Waseminari na Wanovisi anawaalika kujikita katika maisha ya sala kama njia ya kuzungumza na kukutana na Yesu ana kwa ana. Hii ni njia kutoka katika ubinafsi ili kukutana na wengine katika hija ya maisha.

Anasema kwamba, anatamani kuona Kanisa ambalo ni la Kimissionari, tayari kusoma alama za nyakati na kujitosa kimaso maso kwa ajili ya Uinjilishaji wa kina, unaomgusa mtu mzima: kiroho na kimwili, changamoto kwa vijana kushiriki kikamilifu katika mchakato huu, daima wakionesha uaminifu katika ile njia iliyooneshwa na Kristo mwenyewe. Wawe ni watu wa sala, tafakari ya Neno la Mungu na matendo ya huruma; watu wanaotafuta utakatifu wa maisha kwa njia ya Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko aliwaalika Waseminari na Wanovisi, kila mmoja kusali Sala ya Baba Yetu katika lugha yake mwenyewe, kwani kwa pamoja wanaunganishwa na Imani katika Kristo na Kanisa lake!

Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.