Utandawazi usiojali umepelekea watu kushindwa kusikiliza kilio na mahangaiko ya wakimbizi
na wahamiaji wanaokufa maji baharini!
Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 8 Julai 2013 ameadhimisha Ibada ya Misa
Takatifu kwenye Kisiwa cha Lampedusa, Kusini mwa Italia kama kielelezo cha mshikamano
na wakimbizi pamoja na wahamiaji wanaopoteza maisha yao baharini, jambo ambalo limeendelea
kujitokeza mara kwa mara, kiasi kwamba, si habari tena kwa vyombo vingi vya habari.
Baba Mtakatifu amewashukuru na kuwapongeza wananchi wa Kisiwa cha Lampedusa
na wadau mbali mbali kwa moyo wa upendo na mshikamano kwa wakimbizi na wahamiaji wanaotafuta
hifadhi ya maisha kisiwani hapo. Amewakumbuka wahamiaji wa dini ya Kiislam ambao wanaanza
Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, anawatakia kheri na baraka katika Kipindi cha
Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Baba Mtakatifu katika mahubiri yake,
alipenda kuasha dhamiri za watu, ili waweze kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko
ya wakimbizi na wahamiaji; kama binadamu wanaweza kukosea, lakini bado wanabaki kuwa
ni ndugu zao, wanaopaswa kupendwa na kuheshimiwa. Hii ni changamoto ya kuepuka utamaduni
wa kifo, kama ilivyojionesha kwa kiburi cha Kaini aliyetaka kujifananisha na Mungu
na matokeo yake akamuua ndugu yake. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaalikwa
kulinda, kutunza na kudumisha kazi ya uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemkabidhi mwanadamu.
Baba
Mtakatifu anasema, ndugu ni mtu yeyote anayehitaji msaada na faraja katika magumu
na changamoto anazokabiliana nazo. Mtu anayetamani kuboresha maisha yake kwa kupata
ajira na maisha bora zaidi, lakini kwa bahati mbaya, watu hawa wamekumbana na kifo,
hawapati fursa ya kupokelewa, kuonja faraja na ukarimu kutoka kwa watu mbali mbali.
Ni watu ambao wamenyanyaswa na kudhulumiwa na watu wanaojihusisha na biashara
haramu ya binadamu; ni watu wanaoteseka kutokana na umaskini, lakini mbaya zaidi ni
kuona kwamba, kuna kundi kubwa la wahamiaji ambao amefariki dunia wakiwa njiani kuja
Barani Ulaya.
Baba Mtakatifu anasema katika mazingira kama haya, watu wengi
wanajikosha kwa kunawa mikono kutohusika na damu ya wahamiaji na wakimbizi wanaopoteza
maisha yao wakiwa Baharini. Ni mwaliko wa kuwa ni Wasamaria wema kwa kutekeleza wajibu
na dhamana katika maisha kama alivyofanya Yesu, kielelezo cha Msamaria mwema. Jumuiya
ya Kimataifa haina budi kuondokana na utawandawazi usiojali maisha na mahangaiko ya
watu! Mateso yamekuwa ni jambo la kawaida na kwamba, hakuna kinachomgusa mtu!
Baba
Mtakatifu anauliza ni nani kati ya watu waliokuwepo pale, aliyeomboleza kutokana na
vifo vya wakimbizi na wahamiaji baharini? Watu wanaanza kusahau umuhimu wa maisha,
kiasi hata cha kushindwa kusikia kilio cha wale wanaoteseka na kudhulumiwa katika
maisha. Watu wanapaswa kusikitishwa na vitendo vinavyoonesha dhuluma na nyanyaso kwa
jirani zao.
Baba Mtakatifu anasema, ameadhimisha Liturujia ya toba na upatanisho,
kwa kuomba msamaha kutoka kwa Mwenyezi Mungu kutokana na kutojali wala kuguswa na
mateso pamoja na mahangaiko ya ndugu zao wanaopoteza maisha kwa kufa maji baharini.
Baba Mtakatifu ameomba msamaha hata kwa wale wote wanaofanya maamuzi yanayopelekea
mateso na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji, mwaliko wa kusikiliza kilio cha damu
na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji wanaopoteza maisha yao baharini!