2013-07-06 10:02:15

Waseminari na Wanovisi, tumieni vyema kipindi cha malezi, ninyi ni walimu wa imani, matumaini na mapendo!


Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kichungaji, Mwanga wa Imani, anawaalika waamini kusikiliza kwa makini mafundisho ya imani, ili waweze kuwa tayari kutikia wito kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ili kuwamegea wengine zawadi ya imani, inayopaswa kupokelewa kwa unyenyekevu mkubwa, ili iweze kuwageuza kuwa kweli ni mashahidi amini wa Kristo na Kanisa lake; tayari kujitosa kimaso maso kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia. RealAudioMP3

Padre Raymond Saba, Katibu mkuu Idara ya Kichungaji, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika Maadhimisho ya Siku ya Waseminari na Wanovisi, kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani anasema, Waseminari na Manovisi wanapaswa kutambua kwamba, wako katika safari ya malezi yatakayowawezesha kuwa ni walimu wa imani, matumaini na mapendo.

Kipindi cha malezi katika hatua zake mbali mbali kisaidie kuimarisha uelewa na misingi ya imani, inayopaswa kumwilishwa katika uhalisia wa maisha. Walelewa watambua misingi ya imani na mafundisho ya Kanisa. Kanisa linaalikwa kuwasaidia vijana hawa kutambua imani ambayo wanapaswa kwanza kabisa: kuiungama; kuiadhimisha, kuimwilisha kwa kuzingatia amri za Mungu na mwishowe kuisali kadiri ya Kanisa.

Vijana wanaadhimisha Siku hii katika Mwaka wa Imani, ili watambue kwamba, wao ni wadau wakuu wa ushuhuda wa imani kwa sasa na wakati ambapo watakuwa ni Mapadre na Watawa.Vijana hawa watumie vyema kipindi cha malezi na majiundo yao ya maisha ya Kipadre na Kitawa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa kwa sasa na kwa siku za usoni.







All the contents on this site are copyrighted ©.