Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 14 ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji, ninakuleteeni ujumbe wa Neno la Mungu katika Dominika ya 14 ya
Mwaka C. Ujumbe wa furaha ni huu “furahini kwa kuwa majina yenu yameandikwa mbinguni”.
Mpendwa mwana
wa Mungu, katika maisha ya kikristu kwaweza kutokea wasiwasi na mashaka ambayo yaweza
kuleta mmomonyoko wa imani. Kumbe ndiyo maana Mama Kanisa hukaa karibu na watoto wake
akiwaimarisha kwa njia ya Neno la Bwana na kuwashibisha kwa Sakramenti. Jambo la wasiwasi
si la leo bali limewatokea hata wana wa Israeli na hasa walipokuwa utumwani.
Basi
kwa sababu hiyo Mungu aliye mfariji na mwenye huruma kwa watu wake, anamtuma Nabii
Isaya awafariji kwa maneno ya furaha na ya kutia nguvu. Anawaarika akiwaambia washangilie
maana ukombozi utawajia. Aguo hili la kupata uhuru linakamilika katika ujio wa Masiha .
Masiya huyu aliyekuja kwa ajili ya kuleta uhuru na ukombozi kwa watu amejitoa
bila kujibakiza kwa njia ya kifo cha msalaba. Ni msalaba huo ambao katika somo la
II Mt Paulo anasisitiza juu ya utukufu wake dhidi ya vitu vingine vyote ambavyo vyaweza
kuonekana vya maana katika ulimwengu wa leo. Jambo la pili ambalo analikazia katika
kutukuza msalaba ni lile la kuwa kiumbe kipya baada ya kupokea ubatizo. Mambo mengine
ya tamaduni yanakuja baadaye.
Zaidi ya hayo Mtakatifu Paulo anakemea wale
wanaosisitiza kutahiriwa kama njia ya kuwa mkristo, na hivi akazia uhuru kamili katika
kuamua kumfuata Bwana katika uhuru ule wa wana wa Mungu. Kanisa likizikiliza Neno
la Mungu linaratibisha ujumbe huo pia katika sheria za Kanisa kanuni 219 ya kwamba
mkristo anayo haki ya kuchagua kwa uhuru maisha ambayo anajisikia kuwa ameitiwa na
Mungu kuyaishi.
Katika kuutukuza msalaba wa Bwana kuna furaha kuu inayozaliwa
daima kama zawadi ya wokovu kwa Mkristo. Jambo hili tunalipata katika Injili ya Dominika
hii ya 14. Mwishoni mwa Injili Bwana anawaambia wale wafuasi wake 72, furahini kwa
kuwa majina yenu yameandikwa mbinguni. Kwa hakika anayefanya kazi anatarajia mwishoni
kupata matunda na matunda kwa Mkristo ni hayo ya kuingizwa katika orodha ya watakatifu
wa Mbinguni.
Mpendwa siku hizi tunazo simu za vinganjani, ambazo zaweza kutusaidia
kuelewa furaha hii ya kuwa katika orodha ya mbinguni. Unapompatia rafiki yako au mtu
unayemwamini kuwa ni ndugu, namba ya simu halafu baada ya muda unampigia na anakuuliza
wewe nani? Daima unakata tamaa na kujiuliza juu ya uhusiano kama ni wa kweli au vipi?.
Kwa hakika, matarajio yalikuwa kwamba awe ameiingiza namba yako katika simu
yake kama kielelezo kidogo cha mapendo. Basi mwinjili akinukuu maneno ya Bwana ataka
tuelewe juu ya upendo wa Mungu kwa wanadamu ulivyo mkubwa kupita hata uwezo wetu.
Hawa ndugu 72 walikuwa wanafikiria juu ya kutiiwa na pepo lakini Bwana anaonesha jambo
kubwa zaidi ya hilo. Bwana anapopokea namba za simu zetu yaani kwa njia ya ubatizo
mara anaziingiza katika simu yake na kamwe hazitoki humo mpaka kwa ombi letu rasmi
yaani sisi wenyewe kwa uhuru wetu tunaamua kumwacha!
Basi mpendwa mwana wa
Mungu, tujiulize sisi majina yetu yameandikwa wapi? Na yameandikwa kwa kalamu ya
mti au kwa kalamu ya wino? Je, yameandikwa kwenye vitabu vya wapiga kura au vitabu
vya wagonjwa? Je yameandikwa labda katika moyo wa mtu fulani? Kwa hakika yaweza kuwa
katika vitabu hivyo lakini haitaweza kutupa furaha ambayo Nabii Isaya na Mwinjili
wanatuambia katika Liturujia ya Neno la Mungu. Inafaa yawe yameandikwa katika moyo
wa Mmoja anayetupenda kwa Milele yote! Fikiri na kuwaza juu ya Neno Milele Mkristo
we! Kwa maana hiyo si katika Agenda za mikutano bali katika moyo wa Mungu.
Ili
tuweze kukaa katika moyo wa Mungu zipo kazi na nyajibu za kutekeleza daima kadiri
ya Mwinjili. Wajibu wa kwanza ni kusali ili Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika
shamba lake. Watakapokuwa wameingia katika shamba lake lazima wapeleke Injili ya Bwana
na si mambo yao wenyewe, ndiyo kusema waachane na mambo yanayowachelewesha kufanya
kazi ya Bwana. Wanatakiwa daima kupeleka amani na mapendo katika familia na mahali
pote pa uchungaji wao. Wanaalikwa kuwatunza wagonjwa na wenye njaa.
Katika
kupeleka Neno la Bwana kutakuwa na kukataliwa na hata kupigwa, kumbe, wakumbuke hayo
yalimpata Bwana, na hivi waende sehemu nyingine na kazi ya Bwana inasonga mbele. Hawa
wenye kukataa watapata mwanga polepole. Kwa kifupi maisha ya kupeleka Habari njema
ni kutoa ushuhuda wa maisha katika kuamini kuliko kina na kwa kila siku kama atuaambiavyo
Mtakatifu Luka yakuwa msalaba unatakiwa kuchukuliwa kila siku ya maisha yetu.
Mpendwa,
tukitenda kwa upendo mkamilifu basi majina yetu yataweza kuandikwa katika moyo wa
Mungu na hapa ndipo kuna furaha ya kweli na uzima wa milele. Nikutakie yote mema
katika kujitahidi kupeleka habari njema kwa mataifa ili jina lako lipate kuandikwa
katika orodha ya Watakatifu wa mbinguni. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii
imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C.PP.S