2013-07-04 08:17:58

Sadaka ya Misa Takatifu asubuhi ni fursa ya Papa kuzungumza na watu wa nyumbani kwake!


Ibada za Misa Takatifu zinazoadhimishwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa asubuhi na baadhi ya waamini, lakini hasa zaidi na wafanyakazi kutoka Vatican zinalenga kumsaidia Baba Mtakatifu kuwafahamu walau baadhi ya wafanyakazi wa Vatican na kujenga familia ambayo inalihudumia Kanisa la Kiulimwengu. RealAudioMP3
Idadi ya waamini wanaohudhuria Ibada za Misa ya Asubuhi kwa kawaida hazizidi waamini 50 ni kwa ajili ya utashi wa Baba Mtakatifu mwenyewe na kwamba, si kila mwamini anaruhusiwa kuhudhuria.
Ufafanuzi huu umetolewa hivi karibuni na Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican baada ya kupokea mamombi kutoka kwa makundi ya waamini walioonesha nia na utashi wa kuhudhuria Ibada ya Misa Takatifu zinazoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican. Kutokana na mwelekeo huu, Ibada hizi haziwezi kutangazwa moja kwa moja kwenye Luninga au kupitia Radio Vatican.
Mahubiri yanayotolewa na Baba Mtakatifu ni tafakari ya moja kwa moja na ikumbukwe kwamba, Kiitalia si lugha mama ya Baba Mtakatifu Francisko, kumbe kuna haja ya kuielewa ugumu unaoweza kujitokeza. Kwa kuandika mahubiri yake, hii ingekuwa pia ni kazi pevu pengine kuweza hata kumnyima uhuru wa Baba Mtakatifu mwenyewe kuelezea kile ambacho kimemgusa na ambacho angependa kuwashirikisha waamini wakati huo!
Hata hivyo Padre Federico Lombardi anafafanua kwamba, utajiri wa mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko unapatikana kwa kina na mapana kwenye Gazeti la Kila siku la L’Osservatore Romano na Radio Vatican inatoa muhtasari wa mahubiri haya. Kituo cha Televisheni cha Vatican, CTV walau kinajitahidi kutoa muhtasari wa picha na sehemu ya mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko.
Kuna haja kwa waamini kutambua maana ya Maadhimisho binafsi na yale ya hadhara. Pale ambapo ambapo Baba Mtakatifu anapaswa kuhubiri mbele ya umati mkubwa wa watu, mahubiri yake yanapaswa kuandikwa na kuhaririwa, lakini anaposali na kikundi cha ”watu wa nyumbani mwake” anapata fursa ya kuwamegea utajiri wa Neno la Mungu kadiri Roho wa Bwana anavyomkirimia kwa wakati huo!
Padre Federico Lombardi anahitimisha ufafanuzi huu kwa kusema kwamba, uamuzi huu unaheshimu utashi na matakwa ya Baba Mtakatifu Francisko pamoja kuwapatia nafaasi waamini wengi zaidi kuendelea kufaidi mahubiri yake kwa njia za mawasiliano ya kisasa.








All the contents on this site are copyrighted ©.