2013-07-03 08:47:29

Hija ya mshikamano na wahamiaji wanaokufa maji baharini!


Baba Mtakatifu Francisko kwa kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaokimbilia Barani Ulaya wakiwa na tumaini la kupata maisha bora, lakini wanakumbana na kifo maji, Jumatatu, tarehe 8 Julai 2013 atatembelea Kisiwa cha Lampedusa, kilichoko Kusini mwa Italia, kama alama ya mshikamano wa dhati na watu wote wanaoteseka kutoka na vita, kinzani na majanga asilia.

Ratiba iliyotolewa mjini Vatican inaonesha kwamba, Baba Mtakatifu ataondoka kutoka kwenye Kiwanja cha Ndege za Kijeshi, Ciampino majira ya saa 2:00 asubuhi na anatarajiwa kutua kwenye Uwanja wa Ndege wa Lampedusa saa 3:15 na kupokelewa na Askofu mkuu Francesco Montenegro wa Jimbo kuu la Agrigento pamoja na Mstahiki Meya Giuseppina Nicolini wa Lampedusa.

Baadaye, Baba Mtakatifu katika safari hii ya kichungaji kwa mara ya kwanza nje ya Roma atasafiri kwa gari hadi mahali panapojulikana kama Cala Pisana, hapo atapanda Boti kuelekea Kisiwa cha Lampedusa. Akiwa kisiwani hapo, ataungana na wavuvi wakiwa kwenye mashua na boti zao kwenda kutupa shada la maua kwa ajili ya kuwakumbuka wale wote waliopoteza na wanaoendelea kupoteza maisha yao baharini wakiwa na tumaini la kuokoa maisha yao kutokana na vita, maafa asilia au migogoro ya kidini, kisiasa na kijamii au wale wanaotamani kuboresha maisha yao ili kuwa na uhakika wa leo na kesho bora zaidi.

Baba Mtakatifu atawatembelea na kuzungumza na wahamiaji wanaohifadhiwa kwenye Kituo cha "Punta Favolo". Majira ya saa 4:00 anatarajiwa kuanza kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu na baada ya Misa, ataondoka na kuelekea kwenye Parokia ya Mtakatifu Gerlando kwa mapumziko mafupi. Saa 6: 45 ataondoka kwa ndege kurudi mjini Roma na hatimaye, Mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.